Mkurugenzi wa Idara ya Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Dkt. Rashid Mfaume, amewataka Waganga wafawidhi wa vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi kuweka mikakati yenye tija kukabiliana na dosari mbalimbal zinazokwamisha vituo vyao katika matumizi ya mifumo inayobuniwa na OR – TAMISEMI kwa lengo la kurahisisha na kuboresha utolewaji wa huduma za afya kwa wananchi.
Dkt. Mfaume ametoa agizo hilo wakati akihoji sababu za baadhi ya mikoa kushika nafasi ya mwisho kwenye matumizi ya mfumo ulioboreshwa wa usimamizi na uendeshaji wa vituo vya kutolea huduma za afya ya ngazi ya msingi wa ukusanyaji wa taarifa na mapato wa GOTHOMIS, wakati wa mkutano wa mwaka wa Waganga Wafawidhi wa vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi, unaoendelea katika ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.
Kwa mujibu wa Dkt. Mfaume, licha ya mkutano huo kuwa fursa ya kujadiliana juu ya changamoto, mafanikio na masuala kadha ya kitaaluma kuhusu kada hiyo, lakini pia mkutano huo unatumika kupima utendaji kazi wa Waganga Wafawidhi ili kuboresha utendaji kazi wao na kuondoa dosari mbalimbali zinazotatiza utolewaji wa huduma bora kwa wananchi.
Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA OR – TAMISEMI, Bw. Erick Kitali, juu ya utendaji kazi wa mikoa kupitia mfumo wa GOTHOMIS mpaka kufikia mwezi Aprili mwaka 2025, mkoa wa Ruvuma umeibuka kinara ukifuatiwa na Songwe, Mbeya, Kigoma na Singida, huku mikoa mitano ya mwisho ikiwa ni Tabora, Pwani, Shinyanga, Njombe na Iringa ikishika mkia.