Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Altbert Chalamila amesema Mwenge wa Uhuru 2025 unaokimbizwa katika Mkoa huo kwa umbali wa KM 35.03.
Amesema hayo wakati akipokea Mwenge wa Uhuru, ukitokea Mkoa wa Lindi leo Juni 1, 2025 katika Stendi ya Mabasi ya mwendo kasi Mbagala Wilaya ya Temeke Jijini humo.
RC Chalamila akiongea wakati wa mapokezi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025 amesema Mkoa wa Dar es Salaam utakimbiza Mwenge wa Uhuru katika umbali wa KM 357.03 kwa kupitia Miradi 36 yenye thamani ya Tsh.79, 255,160,719.44 (Shilingi Bilioni Sabini naTisa, Milioni Mia Mbili Hamsini na Tano, Laki Moja na Elfu Sitini Mia Saba Kumi na Tisa) Miradi hii ipo iliyokamilika na mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Vilevile, Mwenge wa Uhuru utakapokuwa unapita, utakuwa ukihamasisha shughuli mbalimbali za maerndeleo, upendo, amani, mshikamano na uzalendo kwa Wananchi. Aidha Mbio za Mwenge wa Uhuru zitahamasisha Wananchi kuhusu kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu kwa maendeleo ya Taifa letu.
RC Chalamila pia amesema Mkoa huo unaungana na Watanzania wote katika kuupokea Ujumbe wa Mbio za Mwenge wa Uhuru wa mwaka 2025 unaolenga kuwaelimisha na kuwahamasisha Wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kujitokeza na kushiriki Uchaguzi Mkuu kwa amani na utulivu chini ya kauli mbiu isemayo, *JITOKEZE KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU WA MWAKA 2025* KWA AMANI NA UTULIVU. Pamoja na Ujumbe wa kudumu wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kuhusu Mapambano dhidi ya: VVUIUKIMWI, Malaria, Dawa za Kulevya, Lishe na Rushwa. Ambapo amesisitiza ni vyema tukaendelea kujikinga na magonjwa hayo hatari pamoja na kupambana na Rushwa na Dawa za kulevya katika jamii zetu.
Sanjari na hilo RC Chalamila amesema Mkoa huo utakimbiza Mwenge wa Uhuru ukianzia Wilaya ya Temeke leo tarehe 01/06/2025 na kufuatiwa na Wilaya ya Kigamboni tarehe 02/06/2025, Wilaya ya llala tarehe 03/06/2025, Wilaya ya Kinondoni tarehe 04/06/2025 na kumalizia na Wilaya ya Ubungo tarehe 05/06/2025 kabla ya kuukabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Mkoa wa Tanga tarehe 06/06/2025.
Mwisho Mhe Mkuu wa Mkoa kwa niaba ya Wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam amewakaribisha Wakimbiza Mwenge Kitaifa, ambapo amesema Mwenyezi Mungu awalinde na kuwbariki katika safari yao waliyoianza leo ya kukimbiza Mwenge wa Uhuru katika Mkoa huo, na ametoa rai kwa Wakazi wa Dar es Salaam kuwa tayari kutoa Ushirikiano mkubwa kuanzia leo hadi siku ya mwisho tutakapo ukabidhi Mwenge huu wa Uhuru kwa Mkoa wa Tanga tarehe 06/06/2025.