OR – TAMISEMI
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia afya Prof. Tumaini Nagu amewaelekeza Waganga Wakuu wa Mikoa (RMO’s) kuhakikisha wanasimamia upatikanaji wa ithibati katika maabara za hospitali zote za Halmashauri zilizopo katika Mikoa yao.
Prof. Nagu ametoa maelekezo hayo wakati wa kikao cha majumuisho wa ziara yake ya usimamizi shirikikishi katika Mkoa wa Pwani kilichofanyika katika Halmashauri ya mji wa kibaha mkoani hapo.
“Ithibati ndio alama ya ubora, ukiwa nayo maana yake wewe umekidhi vigezo hivyo huduma zako ni bora, hivyo tunaanza na maabara zote katika ngazi ya afya msingi kuhakikisha tunapata ithibati ya ubora wa huduma zetu” amesisitiza
Aidha, Prof. Nagu amewataka watumishi kutoa huduma zenye ubora kwa kuzingatia miongozo (SOP) ya utoaji wa huduma katika maeneo ya kazi.
“Lazima tuzingatie miongozo ya utoaji wa huduma. Hivyo naelekeza standard operation procedures (SOP’s) zipatikane katika maeneo husika na zitumike kuhakikisha huduma zinazotolewa ni bora. Aidha, vifaa kinga (PPEs) zipatikane na zitumiwe na watoa huduma hususani katika maeneo kama ya kutakasia nguo, maabara, chumba cha kuhifadhi maiti pamoja na maeneo ya kuchoma taka” amesema Prof. Nagu.
Prof. Nagu pia, ameelekeza upimaji wa maeneo yote ya kutolea huduma za afya na kupata hati ya umiliki wa aridhi ili kuondoa changamoto ya migogoro ya ardhi.