Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanikiwa kuwarejesha salama nchini Watanzania 42 kutoka nchini Israel na Iran kufuatia vita vilivyokuwa vikiendelea baina ya mataifa hayo mawili.
Akizungumza mara baada ya kuwapokea Watanzania hao kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo amesema zoezi la kuwarejesha Watanzania wote salama nchini ni utekelezaji wa agizo maalumu la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuhakikisha kwamba Watanzania wote waliopo katika mataifa hayo mawili wanarejeshwa nchini salama.
Aidha Balozi Shelukindo amesema leo juni 25, 2025 wameingia Watanzania makundi mawili, kundi moja liliwasili mchana wa leo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume na kwamba gharama zote za kuwarejesha Watanzania hao zimegharamiwa na serikali na kuongeza kuwa Watanzania wengine kutokea nchini Iran wanatarajiwa kuwasili nchini kesho Juni 26, 2025.
Balozi Shelukindo pia kupitia hadhara hiyo, ametoa rai kwa Watanzania wote kuhakikisha kwamba tunaendelea kuilinda tunu yetu ya utulivu na amani kama ambavyo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyotuasa mara kwa mara.
Akizungumza katika mapokezi hayo, mmoja kati ya wanafunzi waliokuwa wanasoma nchini Israel Bi. Neema Dasina amesema hali ya usalama nchini Israel ilikuwa mbaya kufuatia milipuko ya mabomu ya mara kwa mara isipokuwa kupitia maelekezo mahususi kutoka kwa ubalozi wa Tanzania nchini humo na ule wa nchini Misri, huku akiishukuru serikali na Mhe. Rais Samia kwa kwa ujumla jinsi ambavyo wameonyesha thamani ya Watanzania hasa katika kipindi hiki cha hatari iliyokuwa mbele yao.
Mama mzazi wa mmoja wa vijana waliorejea salama kwa niaba ya wazazi wengine Bi. Asela Luena, ameishukuru serikali ya Mhe. Rais Samia kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa juhudi za dhati za kuwapigania watoto wao, na kuhakikisha kwamba wanarejea salama na kuungana na familia zao.
“baada ya kupata taarifa za hali ya usalama nchini Israel hatukulala usingizi, niliwasiliana na binti yangu, aliniambia mama usiwe na wasiwasi kwasababu sisi wote tupo kwenye mikono salama, serikali imeingilia kati na kila kitu tunafanyiwa na serikali, kwakweli sisi wazazi tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia kwa upendo wake wa dhati kwa taifa letu, tumefarijika sana kama familia lakini kama taifa hii ni heshima kubwa duniani” alimalizia mama Asela Luena.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imefikia uamuzi huo wa kuwarejesha Watanzania wote waliopo katika mataifa ya Israel na Iran kufuatia mapigano yaliyozuka baina ya mataifa hayo mawili, japokuwa siku chache zilizopita zilitolewa taarifa za kumaliza vita hivyo vilivyodumu kwa takribani siku kumi na mbili mfululizo.
Viongozi wengine walioambatana na Katibu Mkuu Balozi. Dkt. Samwel Shelukindo katika mapokezi hayo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, ni pamoja na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga.