Mwakilishi wa Kaimu Meneja Mkuu wa Kampuni ya ETDCO, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi wa kampuni hiyo, Mhandisi Dismas (wa pili kutoka kushoto), akipokea Tuzo ya Heshima ya Sekta ya Ujenzi kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Bw. Gaudence Mmassy. Tuzo hizo zimeandaliwa na Construction Times Gala and Award 2025 kwa lengo la kutambua mchango wa kamapuni mbalimbali zilizofanyika 28 Juni 2025, jijini Dar es Salaam.
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Bw. Gaudence Mmassy akiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa makampuni mbalimbali baada ya kutoa tuzo.
Wafanyakazi wa Kampuni ya ETDCO wakisoma Jarida la Ujenzi ambalo limezinduliwa rasmi kwa ajili ya kutoa taarifa mbalimbali za miradi ya ujenzi nchini.
..
Kampuni ya Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Usafirishaji na Usambazaji wa Umeme (ETDCO) imefanikiwa kupata Tuzo ya heshima ya Mkandarasi Bora wa Ujenzi na Miundombinu ya Umeme pamoja na uendeshaji wa kampuni kutoka Construction Times Gala and Award 2025 zilizofanyika 28 Juni 2025, jijini Dar es Salaam.
Katika tuzo hizo, Kaimu Meneja Mkuu wa ETDCO, CPA Sadock Mugendi, pia ametunukiwa Tuzo ya Uongozi Bora katika Uendeshaji wa Kampuni, ikiwa ni kutambua mchango wake katika kusimamia kwa mafanikio miradi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) wakati wa hafla ya kukabidhi tuzo hizo, iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa Jarida la Ujenzi, Afisa Uwekezaji Mwandamizi wa TIC, Bw. Gaudence Nicholaus Mmassy, amepongeza washindi wote kwa mchango wao mkubwa katika maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.
Akizungumza wakati kupokea tuzo hizo Kwa niaba ya Kaimu Meneja Mkuu wa ETDCO, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi wa Kampuni ya ETDCO, Mhandisi Dismas Masawe, amesema kuwa tuzo hizo ni uthibitisho wa kutambuliwa kwa mchango mkubwa wa kampuni katika ujenzi wa miundombinu ya umeme nchini kwa kuonesha dira ya maendeleo wanayoifuata katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Siri ya mafanikio haya ni usimamizi thabiti kutoka kwa menejimenti ya Kampuni, pamoja na kujitolea kwa dhati kwa wafanyakazi wetu, na utekelezaji wa miradi kwa weledi wa hali ya juu.” amesema Mhandisi Masawe.
Katika tuzo hizo za heshima zilizotolewa na Construction Times, jumla ya makampuni nane yalitunukiwa tuzo hizo za heshima, huku ETDCO ikijivunia kuondoka na tuzo mbili kubwa kutokana na utendaji wake bora, hasa katika usimamizi wa miradi na uendeshaji wa kampuni.