Kibaha, Tanzania – Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imefanya kikao kazi maalum kilichowakutanisha Maafisa Kilimo na Maafisa Maendeleo ya Jamii wote, kwa lengo la kukumbushana wajibu wa kila siku katika kutekeleza majukumu yao ya kiutumishi.
Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Kibaha, kikilenga kuimarisha utendaji kazi, uwajibikaji, ubunifu katika ukusanyaji wa mapato ya ndani pamoja na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha, Dkt. Rogers Shemwelekwa, amewataka watumishi wote kuongeza ubunifu katika kazi zao, kuachana na kufanya kazi kwa mazoea, na kuhakikisha mapato ya ndani yanakusanywa kikamilifu kwa maendeleo ya Halmashauri na wananchi wake.
“Ni lazima tuwe wabunifu katika kila tunalolifanya. Tusifanye kazi kwa mazoea. Wananchi wanategemea huduma bora kutoka kwetu, na sisi ndiyo daraja la utekelezaji wa mipango ya maendeleo,” amesema Dkt. Shemwelekwa.
Kwa upande wake, Afisa Utumishi wa Manispaa hiyo, Bw. Mrisho Mlela, amesema ofisi yake tayari inaendelea kufuatilia kwa karibu utendaji wa watumishi na kuwataka kufuata makubaliano yaliyofikiwa katika kikao hicho, akisisitiza kuwa makubaliano hayo ni sheria inayopaswa kuheshimiwa na kutekelezwa ipasavyo.