OR-TAMISEMI
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemtaka mkandarasi wa Kampuni ya Nyanza Road Works kuongeza kasi ya ujenzi wa Daraja la Mbambe lenye urefu wa mita 81 ili likamilike kwa wakati na kuondoa adha inayowakabili wananchi wa Wilaya ya Rufiji.
Mhe. Mchengerwa akitoa maelekezo hayo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Kijiji cha Mbambe ya kufuatilia maendeleo ya ujenzi wa daraja hilo, amesema; “Mkandarasi ongeza kasi ya ujenzi wa daraja hili kwani asilimia 22 iliyofikiwa bado ni ndogo sana. Kwa mwendo huu, mvua zikiongezeka zitaleta changamoto itakayokwamisha ujenzi.”
Aidha, amewataka wananchi wa Kijiji cha Mbambe kushirikiana na uongozi wa wilaya kwa kutoa taarifa pale wanapoona hali ya kusuasua katika ujenzi wa daraja hilo na kuwahakikishia kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari ametoa fedha kwa ajili ya fidia kwa wote waliopitiwa na mradi huo, ambao unahusisha pia ujenzi wa barabara za maingilio zenye urefu wa kilomita 3.
“Mkuu wa Wilaya, naelekeza Meneja wa TANROADS wa mkoa kuhakikisha kuanzia wiki ijayo fidia inalipwa kwa wale wote waliokwishahakikiwa madai yao. Rais Samia ameshatoa shilingi milioni 500 kwa ajili ya fidia,” ameagiza Mhe. Mchengerwa.
Hata hivyo, Waziri Mchengerwa amewataka wananchi wa Mbambe na Rufiji kwa ujumla kupuuza taarifa potofu kwamba mradi wa daraja hilo umesimama, akisisitiza kuwa ujenzi unaendelea.
Awali, Msimamizi wa Mradi kutoka Kampuni ya Nyanza Road Works, Mhandisi Emmanurel Owoya, amesema kuwa ujenzi huo umefikia asilimia 22, ambapo tayari nguzo za msingi 64 kati ya 107 zimejengwa na Sh.Bilioni 24.16 zitatumika kukamilisha ujenzi wa Daraja la Mbambe, likijumuisha barabara za maingilio za kilomita 3 kwa pande zote mbili za daraja.