*Mbunge wa Kwanza wa kuchaguliwa kwa kura Tanzania ahamasisha Wanawake waache uoga
*Ataka Viti maalumu viwe na ukomo, miaka 10 inatosha
* Kitabu cha The Beijing Journey”, kinachozungumzia safari ya Beijing chazinduliwa
Na Kadama Malunde – Malunde 1 blog
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, wameadhimisha Siku ya Wanawake Duniani mwaka 2025 huku hamasa kubwa ikiwa ni wanawake kujitokeza kugombea nafasi za uongozi na kuondoa vikwazo vya kiuchumi ili kufikia usawa wa kijinsia na haki kwa makundi yote katika jamii.
Mgeni maalum katika maadhimisho haya alikuwa Mhe. Shamim Khan, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa Kiislamu Tanzania (BAKWATA) na Mbunge Mstaafu, ambaye pia alikuwa Mbunge wa Kwanza wa kuchaguliwa kwa kura katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1985, Jimbo la Morogoro Mjini).
Akitoa hotuba yake, Mhe. Khan amehimiza wanawake kujitokeza kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu wa 2025, akisema: “Tunaposherehekea miaka 30 ya Beijing, tunajivunia kuona wanawake wameendelea kuongezeka katika nafasi za uongozi na sasa tunaye Rais Mwanamke Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hata hivyo, bado kuna changamoto kubwa. Wanawake lazima wajitokeze kwa wingi kugombea nafasi za uongozi bila uoga wala aibu”.
Ameongeza kuwa, jamii inapaswa kuacha tabia ya kudhalilisha wanawake, hususan kwenye majukwaa ya kisiasa na mitandaoni, ambapo wanawake mara nyingi wamekuwa wakidhihakiwa na kutukanwa.
Mbali na hilo, Mhe. Khan amezungumzia umuhimu wa kuwepo kwa ukomo wa viti maalumu kwa wanawake katika Bunge, akipendekeza kwamba vipindi vya miaka 10 vinatosha ili vijana wapate nafasi.
“Viti maalumu viwe na ukomo, vipindi viwili miaka 10 inatosha, ni chuo tosha ili tuwape nafasi vijana,” amesema.
Katika hatua nyingine amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kiongozi aliyeitangaza vyema nchi ya Tanzania kupitia Filamu ya The Royal Tour na kuendelea kuhamasisha usawa wa Kijinsia.
Ushiriki wa Wanawake Katika Uongozi: TGNP Yazidi Kuimarisha Haki na Usawa
Mwenyekiti wa TGNP, Bi. Gemma Akilimali, amesema kuwa TGNP itaendelea kufanya kazi ya kuhamasisha wanawake kushiriki zaidi katika uchaguzi na kuongeza kuwa ni muhimu vyama vya siasa viwape nafasi wanawake wengi kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu wa 2025.Mwenyekiti wa TGNP, Bi. Gemma Akilimali
“Tunataka wanawake waingie kwenye vyombo vya maamuzi, mwanamke ni mpangaji mzuri wa rasilimali, na tunataka asilimia 50 kwa 50 katika uongozi,” amesema Bi. Akilimali.
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Bi. Lilian Liundi, ameeleza kuwa ingawa baadhi ya mafanikio yamepatikana tangu Mkutano wa Beijing wa mwaka 1995, bado kuna changamoto nyingi zinazokwamisha maendeleo ya wanawake.
“Vikwazo vya kiuchumi kwa wanawake vinapaswa kuondolewa, na huduma za afya zinapaswa kuboreshwa ili kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi,” amesema Liundi.
Ameongeza kuwa ni muhimu kuhamasisha usawa katika sekta zote, huku akisisitiza kwamba wanawake wanahitaji nafasi zaidi katika maeneo ya uongozi.
UN Women Yapongeza Tanzania kwa Mafanikio ya Usawa wa Kijinsia
Hodan Addou Mwakilishi Mkazi wa UN Women nchiini amezungumzia mchango mkubwa wa TGNP katika kutetea haki za wanawake na kupongeza hatua zilizopigwa na Serikali ya Tanzania katika kufikia usawa wa kijinsia.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa bado kuna changamoto kubwa za kupambana na ukatili wa kijinsia. “Tunaipongeza Serikali ya Tanzania kwa mafanikio makubwa, lakini bado kuna kazi ya kufanya ili kupambana na ukatili wa kijinsia na kuhakikisha wanawake wanapata haki zao zote,” amesema.
Mashirika ya Kimataifa Yasisitiza Ushirikiano wa Pamoja
Wawakilishi kutoka mashirika ya CARE International nchiini, Tanzania, Crossroads International, UNDP na Aghakan Foundation wamekubaliana kuwa ushirikiano wa pamoja unaohusisha wanaume na wanawake, ni muhimu ili kufikia jamii yenye usawa wa kijinsia.
“Tuendelee kupaza sauti ili kufikia jamii yenye usawa, tunataka kesho iliyo bora zaidi,” amesema Nestory Mhando kutoka Aghakhan Foundation na Harriet Makululu kutoka Crossroads International.
Clara Maliwa kutoka UNDP amesisitiza: “Tushirikiane kwa pamoja kuleta ushirikiano, tuwashirikishe wanaume pia, tunataka ushirikishwaji wa wanawake.”
Mkurugenzi wa CARE International nchini Tanzania, Prudence Masako, amepongeza juhudi za wanawake katika kujikwamua kiuchumi kupitia vikoba na kusema kwamba wao ndio waanzilishi wa mfumo wa VICOBA.
Amesema vikoba vimekuwa na manufaa makubwa kwa wanawake, kwani vimewapa uwezo wa kujitegemea kiuchumi na kuboresha maisha yao akieleza kuwa vikoba ni zana muhimu ya kiuchumi inayowawezesha wanawake kupata mikopo ya kifedha, kuwekeza katika biashara, na kujenga mtandao wa kiuchumi.
Kutafakari Safari ya Beijing: Mafanikio na Changamoto
Maadhimisho haya ya Siku ya Wanawake Duniani 2025 yamekuwa ni fursa ya kutafakari kuhusu safari ya Beijing, miaka 30 baada ya mkutano huo muhimu. Wadau wamejadili kuhusu mafanikio yaliyopatikana katika sekta mbalimbali, ikiwemo afya, elimu, na uchumi. Wamekubaliana kwamba bado kuna changamoto nyingi za kupambana nazo, hasa katika kuhakikisha usawa wa kijinsia na haki za wanawake.
Maadhimisho haya yalilenga pia kuhamasisha wanawake kujitokeza zaidi kugombea nafasi za uongozi, kuondoa vikwazo vya kiuchumi, na kuhakikisha huduma za kijinsia zinaboreshwa ili kuwawezesha wanawake kufanikiwa.
Wamesisitiza umuhimu wa kuongeza ushiriki wa wanawake katika vyombo vya maamuzi na kutokomeza ukatili wa kijinsia ili kufikia jamii yenye usawa na haki kwa wote.
Kauli mbiu ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka 2025 ni “Wanawake na Wasichana: Tuimarishe Haki, Usawa na Uwezeshaji”.
TAZAMA PICHA HAPA CHINI


