Singida
Serikali inaendelea kuhakikisha kwamba barabara ambazo zipo katika kila halmashauri ya wilaya zinafunguliwa ili kurahisisha usafiri na usafirishaji katika maeneo ya wananchi.
Hayo yamesemwa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Singida Mhandisi Ibrahimu Kibassa kwenye Maonesho ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi katika viwanja vya Mandewa Mkoani Singida.
Mhandisi Kibassa alisema katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 TARURA ilipangiwa kutumia Sh.bilioni 886.3 ambazo zimefanikiwa kujenga barabara za kilometa 278.32 za kiwango cha lami na kilometa 9334 za kiwango cha changarawe.
Aliongeza kuwa TARURA imekuwa ikitumia teknolojia ya ujenzi wa madaraja kwa kutumia mawe ambapo yapo madaraja 401 nchini na kwa Mkoa wa Singida yapo madaraja 34 yaliyojengwa kwa mawe na mkoa wa Kigoma unashika nafasi ya kwanza kwa kujenga madaraja mengi ya mawe ikifuatiwa na Arusha.
“Ujenzi wa madaraja kwa teknolojia ya mawe tunatumia sana kwasababu gharama zinapungua kwa asilimia 60 ukilinganisha na teknolojia nyingine za kutumia kokoto kama ilivyo kawaida,” alisema.
Alisema kushuka kwa gharama za ujenzi wa madaraja kwa kutumia mawe kunatokana na kwamba mawe hayo yanapatikana kwenye mazingira ya wananchi ambapo nao wananufaika kwa kipato na hivyo kuinua uchumi wao.