Karani Uandikishaji Wapiga kura wapya akimsaidia Mwananchi aliefika Kujiandikisha katika Daftari la Wapiga kura Wilaya ya Mjini Shehia ya Masumbani Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC)Jaji Aziza Iddi Suwedi (watatu kushoto)akiwa pamoja na Makamisna wa Tume hio wakiwa katika Ziara ya Kutembelea Vituo vya Uandikishaji Wapiga Kura Wapya katika Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC)Jaji Aziza Iddi Suwedi akimsikiliza Mmoja kati ya Mawakala wa Vyama vya Siasa wakati alipofanya ziara kutembelea Vituo vya Uandikishaji wapiga Kura Wapya ili kutatua Changamoto zilizo jitokeza Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC)Jaji Aziza Iddi Suwedi akimsikiliza Sheha wa Shehia ya Karakana Juma Makame wakati alipofanya ziara kutembelea Vituo vya Uandikishaji wapiga Kura Wapya ili kutatua Changamoto zilizo jitokeza Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Na Rahma Khamis Maelezo
Zoezi la uandikishaji daftari la wapiga kura awamu ya pili Wilaya ya Mjini linatarajiwa kukamilika Leo Mach 17 huku kukiwa na idadi kubwa ya wananchi waliyojiandikisha katika daftari hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukamilisha zoezi la kutembelea vituo huko Ofisini Maisara Wilaya ya Mjini Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Jaji George Joseph Kazi amesema kuwa kwa Wilaya ya Mjini wamekadiria kuandikisha wapiga kura wapya elfu 78972 .
Aidha amefahamisha kuwa takwimu kamili zitatolewa mara baada ya kukutana na vyama vya siasa kwa ajili ya kupata orodha na taarifa kamili kwa vile zoezi linaendelea hadi kufikia muda wa kufunga vituo.
Akizungumzia kuhusu kupotea kwa kitambulisho ama kuhamisha taarifa za mpiga kura Jaji Kazi amesema kuwa mwananchi afike katika Ofisi ya Tume ya Wilaya husika ili kutafitiwa ufumbuzi.
Amefahamisha hali ya uandikishaji Wilayani humo kuwa zoezi limefanyika kwa amani na utulivu na wananchi wanajitokeza kwa wingi kukiandikisha katika daftari hilo ili kupata haki yao ya kidemokrasia.
Nao Wakuu na Mawakala wa Vituo hivyo wameeleza siku zote za uandikishaji zoezi limekwenda vizuri vituo vimefunguliwa kwa wakati na wananchi wamepata huduma bila ya usumbufu kila mwenye sifa ameweza kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura.
Katika ziara hiyo vituo mbalimbali vimetembelewa ikiwemo Shehia ya Gulioni, Rahaleo, Mnazimmoja Muembeledu, Katakana, Maruhubi, Mwembemakumbi.