Mwamvua Mwinyi, Kibiti
Mkuu wa Wilaya ya Kibiti, Kanali Joseph Kolombo, ametoa onyo kwa baadhi ya watu wanaojihusisha na utoroshaji wa mazao na kusema ni ukiukaji wa sheria unaodidimiza maendeleo ya Wilaya na Mkoa.
Kolombo ameeleza hayo Juni 12, 2025 wakati akizindua rasmi mnada wa kwanza wa zao la ufuta kwa msimu wa mwaka 2025, uliofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti, mkoani Pwani.
Amewataka wakulima kuzingatia taratibu na kanuni za Serikali katika uuzaji wa mazao, akieleza kuwa ni muhimu kuyapeleka kwenye maghala rasmi ili kulinda maslahi ya wakulima na kuchochea mapato halali kwa Halmashauri.
Aidha Kolombo ameagiza taasisi za kifedha kutoa huduma kwa weledi na kurahisisha upatikanaji wa akaunti kwa wakulima ili kuimarisha mzunguko wa fedha katika maeneo ya vijijini.
Amewaasa wanunuzi wa mazao kuhakikisha wanalipa kwa wakati ili kusaidia wakulima kufidia gharama walizotumia katika uzalishaji.
Katika mnada huo wa kwanza, bei ya kilo moja ya ufuta ilifikia sh. 2,414.49, na mnada unaofuata unatarajiwa kufanyika Juni 19, 2025, katika eneo la Kingoma AMCOS, Wilaya ya Mkuranga.
Mnada huo umetajwa kuwa hatua muhimu katika kuinua uchumi wa wakulima wa Mkoa wa Pwani kupitia mfumo rasmi unaolinda haki na mapato ya pande zote.