Na Said Mwishehe
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)Tanzania Bara Stephen Wasira amesema Chama hicho kimebeba maono ya fikra za ukombozi wa watu na kwamba kitaendelea kuwa wakili wa kuwatetea Watanzania na kutatua changamoto.
Wasira ameyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na wananchi wa Jimbo la Busega mkoani Simiyu ambapo amesema Chama hicho ni muungano wa vyama vilivyoleta ukombozi katika nchi uliotokwna na vyama vya TANU na Afro-Shiraz Party (ASP).
“Kwa hiyo wanachama na viongozi wa Chama tunabeba maono ya vyama vilivyopita na sisi ndio tunaendeleza kazi ya uhuru, kuleta mabadiliko katika maisha ya watu.
“Wako watu wengine wako Ulaya wengine wako hapa ‘maajenti’ wao, wanasema CCM imekaa sana nami nawauliza tulivyodai uhuru tulisema tutakaa mpaka lini?
“Tulidai uhuru kwa sababu kuna ajenda ya kubadili maisha ya watu, na kubadili maisha ya watu hakuna mwisho kwa sababu maendeleo yanazaa matatizo mapya.
“Tunaendelea kujenga Tanzania yenye maendeleo kuondoa matatizo.Nataka kuwaambia Chama chetu ni kwa ajili ya kuwakomboa watu ambao hawana uwezo na hata wakipata matatizo hawawezi kuweka wakili, hivyo CCM ndio wakili wao.
“Tunataka Chama hiki kiwe wakili wa watu wote, tuwe tumaini la makundi yote, tunataka liwe tumaini la vijana wa Tanzania, tunataka liwe tumaini la wafanyabiashara, tumaini kwa mama lishe, wamachinga.
Kwa mujibu wa Wasira, CCM ni chama cha wanachi na kuanzia sasa muda mwingi utatumika kuzungumza mambo ya watu.
“Tunataka kutumia muda zaidi kuzungumza mambo yanayohusu watu.Tunataka kujua watu wana matatizo gani na vikao vyetu vizungumze matatizo ya watu na kutatua kero,”amesema Wasira
Amefafanua hata muundo wa mfumo uliopo unataka Chama Cha Mapinduzi kiwe daraja kati ya watu na Serikali ili Chama kijue matatizo ya watu na kimalize yanayowezekana na yanayohitaji dola aagizwe mkuu wa mkoa au mkuu wa wilaya kuhakikisha ufumbuzi wake.
“CCM ni wakala wa watu hivyo tuhakikishe dhuluma hailelewi katika maeneo yetu, Chama
chetu kilipoanza miaka 48 mimi nilikuwa mjumbe katika mkutano ulioanzisha CCM.
“Tulikubaliana kuunda chama chenye nguvu kimuundo na fikra ili kiwakombe watu wanaohitaji ukombozi watu ambao hawawezi kuajiri wakili Chama hiki kiwe wakili wao na hiyo ndio kazi tunayoifanya katika ngazi ya shina hadi halmashauri kuu ya Taifa,”ameongeza.
Hivyo Wasira amesisitiza wana CCM wazungumze mambo yanayohusu maslahi ya watu na wao mtaji wao watu na ukiwanyang’anya watu umekuwa umewanyang’anya mtaji
Kuhusu wagombea ndani ya Chama hicho alisema tayari wameshapata wagombea wao hivyo wanawasubiria watani zao(wapinzani)na kwa hali ilivyo katika vyama vyao Ikulu wataiona kwenye luninga.
“Mpaka hivi ninaposimama hapa hakijapatikana chama mbadala wa kupambana na CCM hata CHADEMA imebakia nusu halafu watushinde.CCM ushindi ni lazima na ushindi unaotokana na kura.”