Naibu Katibu Mkuu wizara ya fedha ,Elijah Mwandumbya akizungumza na waandishi wa habari mkoani Arusha.


Waandishi mbalimbali wa habari wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu mkoani Arusha
…….
Happy Lazaro, Arusha .
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Kodi na Uwekezaji kwa mwaka 2025 litakofanyika Aprili 15 , 2025 katika Ukumbi wa Julius Nyerere International Conventional Center Jijini Dar es Salaam .
Aidha kongamano hilo linatarajiwa kuwa na washiriki wapatao 900 kutoka sekta ya Umma na sekta binafsi,ambapo Kongamano la mwaka huu litaongozwa na kaulimbiu inayosema “Kuongeza Ukuzaji wa Rasilimali za Ndani kwa Kustawisha Fursa za Wananchi”.
Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Arusha leo,Naibu Katibu Mkuu wizara ya fedha ,Elijah Mwandumbya amesema kuwa,Kongamano la mwaka 2023 lilifanyika tarehe 11 Januari na Kongamano la pili lilifanyika tarehe 27 Februari mwaka 2024,Maandalizi ya Kongamano la Kitaifa la Kodi kwa mwaka 2025 yalianza kwa makongamano ya Kodi Kikanda yaliyofanyika kuanzia tarehe 18 Novemba hadi 06 Disemba 2024.
Ameongeza kuwa,Wizara ya Fedha kupitia Kamati ya Ushauri wa Maboresho ya Sera za Kodi (Task Force on Tax Reforms) ina jukumu la kuratibu upatikanaji wa maoni ya wadau, kuchakata maoni hayo na hatimaye kuwasilisha mapendekezo
mbalimbali ya sera za kodi kwenye Kamati ya Ushauri wa Kodi ili yaweze kujumuishwa kwenye maandalizi ya Bajeti ya Serikali ya kila mwaka.
“Utekelezaji wa jukumu hili hufanyika kwa mujibu wa Kifungu cha 10(1) na Kifungu 10(2) vya Kanuni za Bajeti za mwaka 2015, ambapo Wizara ya Fedha hutoa taarifa kwa Umma kuwataka wadau kuwasilisha maoni yao, kama njia ya kuongeza ushirikishwaji wa wananchi.”amesema .
“Kuanzia mwaka 2023, Serikali ilianzisha maazimisho ya siku ya Kongamano la Kodi Kitaifa (National Tax Dialogue) ambayo ni kilele cha jukwaa la ushirikishwaji wa wananchi katika hatua za kupokea mapendekezo ya maboresho ya Mfumo wa Kodi nchini.”amesema Mwandumbya .
Makongamano hayo yalifanyika katika Kanda ya Mashariki (Dar es Salaam), Kanda ya Kaskazini (Arusha), Kanda ya
Ziwa (Mwanza), Kanda ya Magharibi (Kigoma), Kanda ya Kati (Dodoma), Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (Iringa na Mbeya) na Kanda ya Kusini (Mtwara)
Kuanzishwa kwa Kongamano la Kodi kumeleta tija katika maboresho ya mfumo wa kodi ambapo katika maandalizi ya Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2024/25 ushirikishwaji wa wadau uliongezeka zaidi.
Amesema kuwa,Maoni yaliyotolewa yalifanyiwa kazi kwa ujumla na yamewezesha kufanya marekebisho kwenye maeneo mbalimbali ambapo malengo yake ni pamoja na kuendelea kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji, kuchochea
ukuaji wa sekta mbalimbali kama Utalii, Kilimo, Madini, Viwanda, Uvuvi na Ufugaji, kulinda viwanda vya ndani, kuvutia mitaji na uwekezaji nchini, kuongeza ushindani wa viwanda vya ndani, kuchochea ulipaji kodi kwa hiari
na kuboresha usimamizi na ukusanyaji wa kodi, ada na tozo mbalimbali.
Mwandumbya amefafanua kuwa ,upande wa uwekezaji, mwaka 2022: miradi iliyosajiliwa ilikuwa ni 293,
yenye thamani ya shilingi trilioni 11.7.
“Mwaka 2023 miradi iliyosajiliwa ilikuwa ni 526, iliyokuwa na mitaji yenye thamani ya shilingi trilioni 14.6, na
ilitengeneza ajira 53,871. Aidha, mwaka 2024 miradi ya uwekezaji iliyosajiliwa ilikuwa 901, iliyokuwa na thamani ya shilingi trilioni 24.67, na ilitengeneza ajira 212,293.”amesema Mwandumbya.
“Mapato ya ndani kwa mwaka 2022/23 yalikuwa shilingi bilioni 26,2778, mwaka 2023/24 yalikuwa shilingi bilioni 29,830, sawa na ongezeko la asilimia 13.5. Aidha, katika kipindi cha kuanzia Julai 2024 hadi Februari 2025 mapato
ya ndani yalikuwa shilingi bilioni 22,579.”amefafanua Mwandumbya.
Aidha ametoa rai kwa wananchi wote kutumia fursa iliyotolewa na Serikali kwa kila mmoja kutoa maoni na kuwasilisha
mapendekezo yake ya kuboresha sera za kodi.