MKUU wa Mkoa wa Simiyu Kenani Kihongosi amemshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha anatatua kero mbalimbali zinazowakumba wachimbaji wadogo wa madini katika mkoa huo wa Simiyu.
Akizungumzia katika mkutano wake na wachimbaji wadogo wa madini Mkoa wa Simiyu, Kihongosi amesema changamoto kubwa iliyokua inaikabili kada hiyo ni ukosefu wa mitaji na kufanya utafiti wa maeneo yenye madini.
“Tayari Serikali kupitia Wizara ya Madini imeunda Tume Maalum kati ya Sekta binafsi na ya umma kwa ajili ya kufuatulia changamoto zinazowakabili wachimbaji wadogo ikiwemo kuangalia namna wanavyoweza kuwezeshwa mitaji na mbinu za utafiti,” amesema Kihongosi.
Kuhusu umeme ambao ni hitaji la msingi katika maeneo ya migodi, Mkuu wa Mkoa Simiyu amesema, tayari Serikali imetoa Sh.bilioni 90 ili kujenga kituo cha kuongeza nguvu ya umeme kwa lengo la kumaliza changamoto ya umeme kukatika mkoani Simiyu sambamba na kupunguza gharama ya kutumia mafuta ya dizeli wachimbaji.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa aliyekuwa mgeni rasmi katika mkutano huo amesema Serikali itaendelea kufuatilia na kutatua changamoto zinazowakabili wachimbaji nchini lengo likiwa ni kutoa kipaumbele cha kipekee kwa wachimbaji.