NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
TAASISI ya Bloom Wellness Limited imepongezwa kwa kuanzisha na kuzindua Wiki ya Ustawi Tanzania 2025 ambayo itawaleta pamoja wadau ili kuwa na mjadala mpana zaidi kuangazia kwa kina suala la ustawi wa kijamii na kiafya kwa ujumla.
Pongezi hizo amezitoa leo Aprili 30, 2025 Jijini Dar es Salaam, Mtaalamu wa Mawasiliano ya Afya na Mabadiliko ya Tabia katika jamii kutoka Wizara ya Afya Grace Tadei wakati wa uzinduzi wa wiki hiyo ya ustawi.
Amesema magonjwa mengi yasiyo ambukiza yamekuwa yakiongezeka kila uchwao ikichangiwa na kutofuatwa kwa Mrindoko bora wa maisha.
“Magonjwa ya akili, kisukari, shinikizo la damu, ajali na saratani imekuwa changamoto kubwa kwa binadamu, familia na taifa kwa ujumla”. Amesema
Aidha amesema Serikali inahakikisha wafanyakazi wake wanapunguza uwezekano wa kupata magonjwa yasiyoambukiza ndo maana wamekuwa wakitoa elimu kwa njia ya mtandao na kuna wakati wanaitisha watumishi wa serikali kuwapa elimu bure.
Pamoja na hayo amewataka Waajiri nchini kuweka miundombinu mahala pa kazi itakayowawezesha wafanyakazi kufanya mazoezi ili kusaidia kuimarisha Afya ya akili na mwili.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya ustawi wa Afya ya jamii ya Bloom Wellness Sophia Byanaku amesema kupitia wiki ya ustawi wa Afya inayotarajiwa kufanyika julai 1-2 mwaka huu itasaidia kuleta pamoja wadau wa Afya , watafiti na watunga sera ili kujadili ustawi wa Afya hususani magonjwa yasioyoambukiza na kuleta mwamko unaolenga kuleta mabadiliko ya pamoja ya watu kubadilisha Mtindo wa maisha.
Amesema wanaoshiriki wiki hiyo ya ustawi Tanzania ni wadau kutoka kada mbalimbali zinazohusika na lishe, afya ya akili na sekta zisizo za kiserikali.
“Tunataka tuwalete wadau kwa pamoja tuongee, tuone changamoto zipo wapi kwa hili suala na sauti ikitoka kwa pamoja italeta nguvu na tija na itakuwa na mabadiliko kwa wote”. Amesema Byanaku.