MAKAMU wa Pili wa Rais Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdullah amesema, Jukwaa la wakuu wa Taasisi za Umma ni njia moja ya kuwaweka pamoja kujadili changamoto na mafanikio ya serikali lengo kuleta maendeleo ya nchi.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji Sharif Ali Sharif kwa niaba ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Hemed Suleiman Abdullah wakati akizindua Jukwaa la Kwanza la Wakuu wa Taasisi katika ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa ndege Mkoa wa Mjini Magharib Unguja.
Amesema, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka misingi imara ya kiutendaji ambayo huchangia katika taasisi na nchi kwa ujumla ikiwemo utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Amesema Jukwaa hilo ni la kihistoria ambapo kwa mara ya kwanza linafanyika Zanzibar kwani ni hatua nzuri ya kuendeleza maono ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuwataka kuwa wabunifu katika Taasisi wanazoziongoza ili kufikia malengo.
Amefahamisha kuwa Jukwaa hilo ni muhimu katika kuendeleza mashirikiano na mshikamano kwa wakuu hao ili kuibua fursa zitakazoleta tija kwa taifa.
“Kutokana na umuhimu wa kuwepo kwa Jukwaa hilo ni vyema kuendelezwa kila mwaka ili kutoa nafasi kwa wakuu wa taasisi kukaa pamoja na kupata fursa ya kujadiliana mambo mbalimbali kwa maslahi mapana ya taifa” alisema Mhe. Shariff.
Aidha ameeleza kuwa kupitia Jukwaa hilo kutapatikana fursa ya kujadiliana na kubadilishana uzoefu juu ya huduma mbalimbali ambazo taasisi hizo zinatoa huduma.
Hivyo alisema kupitia mjadala huo utawezesha kufanya tathimini ya maendeleo ambayo wangeweza kufikiwa na taasisi hizo pamoja na kuweka kwa kufikia maazimio ya pamoja ili kuziendeleza vyema taasisi kiutendaji na kuongeza ufanisi ambao utaleta mafanikio katika utoaji wa huduma kwa jamii.
Akitoa rai kwa washiriki wa jukwaa hilo kutumia vizuri fursa hiyo ili watakapomaliza mafunzo hayo waweze kuleta mabadiliko ya kimaendeleo katika taasisi wanzoziongoza ili ziendelee kutoa huduma bora.
Amesisitiza kuwa ni muhimu kuzingatia misingi ya utawala bora katika ngazi zote wanazozisimamia ikiwemo kufuata sheria, uadilifu, uwazi na uwajibikaji ili kuepukana na changamoto zinaweza kujitokeza ikiwemo ubadhirifu, rushwa na unyanyasaji kwa wanaowaongoza.
Amewaomba wakuu wa taasisi hao kushiriki uchaguzi kwa amani ifikapo Oktoba 2025, pamoja na kuwakumbusha wanaowaongoza na wananchi kwa ujumla kudumisha amani na utulivu ambayo ndio chachu ya maendeleo endelevu.
Nae Naibu Waziri wa Fedha na Mipango amesema viongozi wakuu wa nchi wamekuwa wakianzisha na kutengeneza mashirika mbalimbali hivyo ni vyema jukwaa hilo kutekeleza lile lengo kwa kukaa pamoja na kukumbushana yale yanayotakiwa kutekelezwa kwenye taasisi.
Aidha amewataka watendaji hao kuwa waaminifu ili kulifisha mbali taifa lakini pia ni vyema kuwa wabunifu kwani Marais wa nchi wanasisitiza kuwa wabunifu na kuacha kufanya kazi kwa mazowea.
Mapema Mwenyekiti wa jukwaa hilo Juma Burhani, alisema miongoni mwa malengo ya jukwaa hilo ni kutengeneza fursa za kibiashara na kimaendeleo zitakazosaidia wananchi wa Zanzibar na Tanzania bara kuchochea uchumi wa maendeleo jumuishi na kuimarisha umoja wa taifa.
Alisema wamejipanga kufanya tathmini kwa taasisi za umma, kuendeleza jukwaa hilo kwa kufanyika kila mwaka ili liendelee kuchochea ufanisi,kuimarisha uwajibikaji na ubunifu.
Kwa upande wake Msajili wa Hazina Zanzibar Waheed Ibrahim Mohamed Sanya amesema maazimio ya Jukwaa hilo yateleta ufanisi na utekelezaji mzuri wenye kuleta tija katika nchi.
Jukwaa hilo la siku tatu litawajumuisha Wakuu wa Taasisi za Umma na Binafsi za Tanzania Bara na Zanzibar ambapo kauli mbiu “Uongozi bunifu na Mashirikiano ni Muhimu ili kufikia Maendeleo Endelevu Zanzibar”.




