Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Kusafirisha na Kusambaza Umeme (ETDCO) wakipokea taarifa ya maendeleo ya mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Katavi, unaotekelezwa na ETDCO na ambao umefikia asilimia 96, wakati wa ziara ya kukagua mradi huo iliyofanyika Juni 19, 2025 Mkoani Tabora.
Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Kusafirisha na Kusambaza Umeme (ETDCO) wakiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa kampuni hiyo katika eneo la mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Katavi, wakati wa ziara ya ukaguzi wa mradi huo iliyofanyika Juni 19, 2025, mkoani Tabora.
………….
Bodi ya Wakurugenzi Kampuni ya Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Kusafirisha na Kusambaza Umeme (ETDCO) imeridhishwa na usimamizi bora wa utekelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Katavi.
Akizungumza Mkoani Tabora wakati wa ziara ya ukaguzi wa mradi huo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Bw. Raymond Mbilinyi, amesema kuwa maendeleo ya mradi yameridhisha, huku akieleza kuwa mpaka kufikia mwisho wa mwezi Juni mwaka huu, umeme kutoka kwenye gridi ya taifa utakuwa umefika Wilayani Mpanda, Mkoa wa Katavi.
“Tumeridhishwa na maendeleo ya mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Katavi, ambapo kwa sasa umefikia asilimia 96” amesema Bw. Mbilinyi.
Kwa upande wake, Kaimu Meneja Mkuu wa ETDCO, CPA. Sadock Mugendi, ameieleza bodi hiyo kuwa ujenzi wa mradi huo unaendelea vizuri na sasa upo hatua za mwisho za ukaguzi wa laini.
Ameongeza kuwa mpaka kufikia mwishoni mwa mwezi Juni 2025, mradi utakuwa umekamilika kwa asilimia 100 na kufikisha umeme Mkoani Katavi.
Naye Mkurugenzi wa TANESCO Kanda ya Magharibi, Mhandisi Richard Swai, amesema kuwa kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika mikoa ya Tabora na Katavi.
Mhandisi Swai amewataka wananchi wa mikoa hiyo kujiandaa kupokea umeme wa gridi ya taifa, ambao utachochea shughuli za kiuchumi na maendeleo kupitia sekta mbalimbali kama kilimo, viwanda, usindikaji na uongezaji thamani wa mazao.