Na Kassim Nyaki, NCAA.
Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imetoa mafunzo ya siku mbili kuanzia tarehe 29 hadi 30 Mei, 2025 kwa wadau wa Utalii kuhusiana na matumizi ya mfumo mpya wa *Safari Portal V2* ulioboreshwa kutoka mfumo wa zamani wa Safari Portal.
Akifungua Mafunzo hayo Kaimu Meneja wa Huduma za Utalii na masoko NCAA, Afisa Uhifadhi Mkuu Peter Makutian ameeleza kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo wadau wote wa Utalii kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa makusanyo ya mapato yatokanayo na shughuli za Utalii ambao umeboreshwa ili kurahisisha utoaji huduma kwa wadau wote wanaofanya kazi na NCAA.
“Tumeboresha mfumo wetu wa makusanyo ya mapato ya Utalii na utaaanza kutumika kuanzia tarehe 31/05/2025, kwa hiyo ni muhimu wadau wetu wanaopata huduma kupitia mfumo huu wawe na uelewa ya maboresho yaliyofanyika na kuwasaidia namna ya kuhamisha taarifa zao kwenye mfumo mpya kabla ya tarehe ya kuanza mfumo huo” alilisitiza Makuatian.
Makutian ameongeza kuwa sababu zilizopelekea kuboresha mfumo huo ni kuendana na mabadiliko ya kukua kwa teknolojia ya habari na mawasiliano sambamba na kuzingatia mapendekezo ya Wadau wa utalii ambao ndio watumiaji wakuu wa mfumo huo.
Mafunzo hayo yameshirikisha makundi mbalimbali katika mnyororo wa sekta ya utalii ikiwemo Waongoza watalii, wamiliki wa kampuni za utalii, madereva wa utalii, wamiliki wa hoteli na wadau wengine wanaohusika na sekta ya Utalii.
Wadau wa utalii walioshiriki mafunzo hayo wametoa pongezi kwa uongozi wa NCAA kwa maboresho ya mfumo huo ambao umerahisisha taratibu za malipo bila kutumia mda mrefu wanapokuwa na shughuli za utalii na wageni ndani ya hifadhi ya Ngorongoro