*Waandishi wa Habari Watakiwa Kuwasilisha Vyeti Sahihi Pekee kwa Ithibati
MAAFISA wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari Bi. Rehema Mpagama, Wakili wa Serikali Mwandamizi na Bw. Mawazo Kibamba, Afisa Habari Mwandamizi anayeshughulikia Ithibati wakifafanua masuala mbalimbali ya Mfumo wa Usajili wa Waandishi wa Habari.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti maafisa hao wamewasisitiza Waandishi wa Habari wanaojisajili katika mfumo huo kupitia kiunganishi cha https://taihabari.jab.go.tz kuzingatia maelekezo yaliyotolewa ikiwemo kupakia kwenye mfumo vyeti vya kitaaluma na siyo vya Elimu nyingine.
Akifafanua kuhusu hilo Bw. Kibamba amesema mwombaji wa Ithibati hapaswi kuweka kwenye mfumo cheti cha kidato cha nne, kidato cha sita, mafunzo na semina za muda mfupi wala vyeti vya taaluma nyingine zisizo na uhusiano na Uandishi wa Habari.
Amebainisha kuwa Waombaji hawapaswi pia kuweka kwenye mfumo viambatisho vya Wasifu Binafsi (CV), vyeti visivyo halali (fake), vyeti vya watu wengine na viambatisho vingine visivyo na uhusiano na mwombaji au taaluma yake.
Kuhusu vyeti vya taaluma, Kibamba amesema vyeti vinavyopokelewa ni vya Diploma ya miaka miwili au digrii ya miaka mitatu ya Uandishi wa Habari, Mawasiliano kwa Umma (PR), Upigaji na Uandaaji wa Video na Picha na ujuzi mwingine katika uandaaji wa maudhui ya Habari.
Kwa Upande wake Wakili Mpagama amesisitiza makundi mengine ya Waandaaji wa Vipindi na Wapiga Picha za mjongeo na kawaida kujitokeza kujisajili kwani hadi sasa waliojisajili ni Waandishi wa Habari na Wahariri wao.