Dar es Salaam. Ofisi ya Msajili wa Hazina ina shauku ya kukusanya Sh1 trilioni kama mapato yasiyo ya kodi katika mwaka huu wa fedha wa 2024/25.
Akizungumza katika kikao na wahariri wa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam Jumatatu, Juni 2, 2025, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu alisema tayari karibia Sh900 bilioni zimekusanywa kutoka taasisi za umma na kampuni ambazo serikali ina umiliki wa hisa chache zipatazo 200.
“Hadi kufikia sasa (Juni 2, 2025) Ofisi ya Msajili wa Hazina imekusanya karibia Sh900 bilioni kama mapato yasiyo ya kodi na matamanio yetu ni kukusanya Sh1 trilioni katika mwaka wa fedha wa 2024/25.” alisema Bw. Mchechu.
Ikiwa Ofisi hiyo itafanikiwa kukusanya Sh1 trilioni, itakuwa ni ongezeko la asilimia 30.4 ikilinganishwa na mwaka wa fedha uliopita ambapo kiasi cha Sh767 bilioni kilikusanywa.
Ili kuhakikisha Ofisi hiyo inafikia adhima hiyo ya kukusanya Sh1 trilioni, Msajili wa Hazina alizitaka taasisi ambazo bado hazijawasilisha gawio zifanye hivyo ndani ya wiki hii.
“Taasisi zote ambazo bado hazijawasilisha gawio kwa serikali, kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina, zinapaswa kufanya hivyo ndani ya wiki hii ili ifikapo siku ya Gawio, Juni 10 mwaka huu, asiwepo wa kudaiwa,” alisema Bw. Nehemiah Mchechu, Msajili wa Hazina.
Bw. Mchechu alisema ukuaji wa mapato yasiyo ya kodi umetokana na kuimarishwa kwa utaratibu wa ufuatiliaji wa karibu wa gawio na michango katika Mashirika ya umma na matumizi ya Mifumo ya TEHAMA.
“Ofisi imefanikiwa kuunganisha Mfumo wa Mpango na Bajeti (PlanRep) na Mifumo ya ERMS na e-Watumishi pamoja na kufanya maboresho ya Mfumo wa MUSE ambao unawezesha kupata taarifa halisi za matumizi katika Taasisi na Mashirika ya Umma ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa fedha za Umma,” alisema Bw. Mchechu
Alisema maboresho hayo sasa yamefanya mifumo kubadilishana taarifa ipasavyo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan aliyetaka kuona mifumo inasomana.