Na Mwandishi wetu, Mirerani .
TAASISI ya Akhsante Foundation Tanzania imechinja ng’ombe 800 mbuzi na kondoo 3,000 kwenye mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
Vitoweo hivyo vinachinjwa kwa ajili ya kusherehekea sikukuu ya Eid El Adha na kugawiwa kwa wahitaji mbalimbali kwa baadhi ya wakazi wa mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro.
Zoezi hilo limesimamiwa na taasisi ya kijamii ya Akhsante Foundation Tanzania ambayo inafanya shughuli zake kwenye maeneo mbalimbali ya Tanzania Bara.
Mwenyekiti wa Taasisi hiyo Katada Hashimu Kimaro amesema mifugo hiyo imechinjwa kwa ajili ya kupatiwa wahitaji mbalimbali katika zoezi hilo litakalofanyika kwa muda wa siku tatu.
Katada amesema makundi mbalimbali yamepatiwa msaada huo wakiwemo wanawake wajane, wanaume wagane, wazee, walemavu, watoto yatima, taasisi za dini na taasisi za serikali.
“Msaada huu umetolewa kwa makundi mbalimbali bila kubagua madhehebu ya dini, rangi, wala kabila kwani lengo ni walengwa wanufaike na kitoweo hiki wakati wa kusherekea sikukuu ya Eid El Adha,” amesema.
Mmoja kati ya wanawake wa mji mdogo wa Mirerani Mwadawa Hassan ambaye amepata msaada huo amewashukuru wahisani hao kwa kuwapatia mboga ambayo wameitumia kupikia kwenye sikukuu ya Eid El Adha.
“Tunawashukuru waturuki kwa kutupa msaada huu kwani tumesherehekea vyema sikukuu hiki kupitia msaada huu wa mboga,” amesema Mwadawa.