Serengeti-Mara.
POLISI Kata wa Kata ya Ikoma Wilaya ya Serengeti mkoani Mara Sajenti Emmanuel, ametoa wito kwa wazazi kutokuwa chanzo cha mmomonyoko wa maadili kwa watoto wao.
Ametoa kauli hiyo wakati akitoa elimu ya Polisi Jamii kwa wananchi wa kitongoji cha Momorogoro kijiji cha Robanda, kata ya Ikoma, katika mwendelezo wa kampeni ya Elimu ya Nyumba kwa Nyumba.
Katika maelezo yake, Sajenti Emmanuel amewakumbusha wazazi kuwa wanalo jukumu kubwa la kuiandaa vyema kesho ya watoto wao kwa kuwapatia malezi bora, ambayo yatawasaidia kuwa watu wenye tija na mafanikio katika nyanja za elimu, afya, na uchumi.
Aidha, aliwasisitiza wazazi kuwafundisha watoto wao kuvaa mavazi ya heshima yanayomstiri mtu, kudumisha usafi wa mwili, mavazi, na mazingira yanayowazunguka, kama njia ya kulinda maadili yao.
Aliwakumbusha wazazi kuwa urithi wa kudumu ambao wanaweza kuwaachia watoto wao ni elimu, alisema itawapatia maarifa muhimu katika kipindi chote cha ukuaji wao na kuwasaidia kuwa watu wanaofaa na kuheshimika katika jamii.