Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inashiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma, ambapo Ofisi hiyo imejikita katika kutoa huduma za Ushauri wa Kisheria, Elimu ya Sheria, Utatuzi wa Migogoro pamoja na kushughulikia malalamiko ya Wananchi na Wadau.
Akizungumzia kuhusu ushiriki wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika Maadhimisho hayo Wakili wa Serikali Bi. Catherine Paul amesema kuwa lengo la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kushiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi ni kutoa huduma za Kisheria kwa wananchi pamoja na kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali yanayotekelezwa na Ofisi hiyo.
“Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali iko katika maadhimisho haya kwa lengo la kutoa huduma za Kisheria kwa Wananchi, tutakuwa hapa takribani wiki nzima tukiwahudumia wananchi.” Amesema Bi. Catherine
Katika hatua nyingine Bi. Catherine ametoa wito kwa Wananchi wa Mkoa wa Dodoma na maeneo ya jirani kutembelea banda la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali lililoko katika Maadhimisho hayo ili waweze kupata elimu kuhusu Sheria na kutatuliwa changamoto mbalimbali za kisheria zinazowakabili.
“Nichukue nafasi hii kuwakaribisha wananchi wote wa Dodoma kutembelea katika banda letu lililopo hapa Chinangali tuko tayari kuwahudumia.” Amesema Wakili Catherine
Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yalianza tarehe 16 Juni, 2025 yanafanyika hadi tarehe 23 Juni, 2025 katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma, ambapo Maadhimisho hayo yamebeba Kauli mbiu isemayo Himiza matumizi ya mifumo ya kidijiti ili kuongeza upatikanaji wa taarifa na kuchagiza uwajibikaji