Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipoweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Amali ya Mwamapalala iliyopo Wilaya ya Itilima mkoani Simiyu. Rais Mhe. Dkt. Samia ameweka jiwe hilo la msingi leo tarehe 18 Juni,2025 kwa niaba ya shule zote 103 za Sekondari za Amali zinazojengwa kote nchini.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Amali ya Mwamapalala iliyopo wilayani Itilima mkoani Simiyu. Rais Mhe. Dkt. Samia ameweka jiwe hilo la msingi kwa niaba ya shule zote 103 za Sekondari za Amali nchini tarehe 18 Juni, 2025.
………………
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali ya CCM anayoiongoza, imechukua hatua madhubuti katika kuweka mwelekeo wa elimu itakayotoa ujuzi na stadi za kazi kwa vijana ili kuwapatia sifa katika soko la ajira.
Rais Samia amesema hayo leo Jumatano, tarehe 18 Juni 2025, wakati alipoweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Amali ya Sekondari Mwamapalala, Wilaya ya Itilima, kwa niaba ya shule zote 103 za sekondari za amali zinazojengwa maeneo mbalimbali, nchini.
“Shule hizi na elimu ya ufundi stadi tunalenga zitoe elimu ya ujuzi kwa vijana wetu ili wanapomaliza wawe na sifa katika soko la ajira, kuajiriwa au kujiajiri. Shule hii tutaanza masomo ifikapo mwezi Januari mwakani,” alisema Rais Samia. Rais Dkt. Samia pia aliwapongeza wananchi wa Itilima jinsi wilaya yao inavyopiga hatua za maendeleo kwenye sekta mbalimbali, huku akiwasisitiza umuhimu wa kuwapatia watoto wao fursa za kupata elimu, wakitumia ipasavyo miundombinu inayojengwa kwa gharama kubwa na Serikali yao.
“Ndugu wananchi wenzagu wa Itilima kwanza nawapongeza sana kwa hatua kubwa za maendeleo mliyonayo. Leo nimeweka jiwe la msingi kwa niaba ya shule zingine zote za amali zinazojengwa nchini. Nitakapozindua zikikamilika kujengwa, pia nitazindua kwa niaba ya shule zote nchini.
Mhe. Rais Dkt. Samia anaendelea na ziara yake yake ya kikazi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Simiyu, leo ikiwa ni siku ya nne tangu alipoanza siku ya Jumapili, tarehe 15 Juni 2025.l