Waziri wa Uchukuzi wa Anga wa Jamhuri ya Somalia, Mhe Mohamed Nuh Juni 30, 2025 amefanya ziara katika Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania kuangazia fursa mbalimbali za ushirikiano wa kiuchumi katika sekta ya anga.
Mhe. Nuh ameongoza ujumbe wa Somalia katika mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Bw. Salim Msangi akiongozana na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) Inj. Peter Ulanga ambapo wamejadili fursa za ushirikiano katika usafiri wa anga na mafunzo ya usafiri wa anga kati ya Tanzania na Somalia.
Kwa upande wake Bw. Msangi ameeleza kuwa TCAA inaendelea kupanua Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC) na kusisitiza kuongeza nguvu katika kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizi katika masomo ya anga. Aidha, ameshukuru kwa idadi ya wanafunzi kutoka Somalia wanaochukua kozi chuoni hapo.
Katika hatua nyingine, Somalia imeeleza kuwa ni iko tayari kuboresha ushirikiano wa uwili na Tanzania katika Sekta ya Usafiri wa Anga.
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Afrika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Ellen Maduhu pamoja na watendaji kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na TCAA.