Baadhi ya wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi katika Maonesho ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) wameonesha kuridhishwa na huduma zinazotolewa na wizara hiyo.
Wakizungumza katika banda la Wizara ya Ardhi tarehe 4 Julai 2025 katika maonesho hayo yanayoendelea katika viwanja vya Mwl Nyerere Dar es Salaam, wananchi hao wamesema, huduma zinazotolewa ni nzuri na za haraka ukilinganisha na zile zinazotolewa ofisini.
Wametolea mfano wa huduma ya utoaji Hati Milki za Ardhi pamoja na ukadiriaji kodi ya pango la ardhi kuwa, ni moja ya huduma inayopatikana kwa haraka jambo linaloonesha kuwa, wizara imejipanga katika maonesho hayo.
“Tunaomba wizara iendelee kuboresha huduma zake ili kujenga imani kwa wananchi na serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania” wamesema.
Katika maonesho hayo yaliyobeba kaulimbiu ya “Fahari ya Tanzania” Wizara ya Ardhi inatoa huduma za Hati Milki za Ardhi, Ubadilishaji jina (Deed poll), Ukadiriaji Kodi ya Pango la Ardhi, ushauri kuhusina na Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya pamoja na utatuzi wa changamoto za sekta ya ardhi.
Aidha, huduma za sekta ya Ardhi katika manispaa zote za mkoa wa Dar es salaam za Kinondoni, Ubungo, Kigamboni, Ilala na Temeke zinapatikana
Vile vile, elimu kuhusiana na masula ya sekta ya milki, urasimishaji pamoja na namna ya kujiunga na Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) katika masomo kwa ngazi ya Astashahada na Stashahada inatolewa na wataalamu sambamba na kutoa fomu za kujiunga na chuo hicho.