Bohari ya Dawa (MSD) leo imefanya kikao muhimu na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), Mheshimiwa Elias M. Magosi, ambaye pia ni Katibu Mtendaji wa SADC, kikao hiko kiliongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, kilikuwa na lengo la kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika sekta ya afya.
Katika kikao hicho, pande zote mbili zilijadiliana kuhusu mikakati ya pamoja ya kuboresha upatikanaji wa bidhaa za afya ndani ya ukanda wa SADC, kuongeza usalama wa bidhaa za afya, pamoja na kushirikiana katika maeneo ya uzalishaji, utafiti, na usambazaji wa dawa.
Akizungumza katika kikao hicho, Mavere Tukai, Mkurugenzi Mkuu wa MSD, alieleza dhamira ya taasisi hiyo kushirikiana na nchi wanachama wa SADC kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa bora za afya kwa gharama nafuu. “Tunaamini kuwa kupitia ushirikiano huu wa kikanda, tutaongeza uwezo wa pamoja wa kiutendaji, kuongeza ufanisi wa manunuzi na kurahisisha usambazaji wa dawa na vifaa tiba kwa wananchi wetu,” alisema Tukai.
Aidha kwa upande wake, Mheshimiwa Elias M. Magosi alipongeza juhudi za MSD katika kuhakikisha huduma bora za afya nchini na kueleza kuwa mafanikio hayo yanatoa mfano bora kwa nchi nyingine wanachama wa SADC. “MSD imeonyesha kiwango cha juu cha uwajibikaji, ubunifu, na weledi—na kwa kweli ni taasisi ya kuigwa ndani ya ukanda wa SADC. Tunaipongeza kwa mafanikio haya na tuna matumaini makubwa ya kuimarisha ushirikiano wetu katika kuleta mageuzi chanya kwenye sekta ya afya kwa nchi wanachama,” alisema Magosi.
Kikao hiki ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kuhakikisha wananchi wa ukanda wa SADC wanapata huduma bora za afya kupitia mashirikiano ya kimkakati kati ya taasisi za serikali.