Na Mwandishi wetu, Babati
GHALA kubwa jipya la mazao lililopo Kata ya Mamire Wilayani Babati Mkoani Manyara, linalomilikiwa na mwekezaji Herman Mandoo litatochea fursa ya kiuchumi kwa wakulima wa eneo hilo na majirani.
Mmiliki wa ghala hilo, mwekezaji Mandoo amesema ghala hilo jipya lenye uwezo wa kuhifadhi tani 1,000 hadi 1,300 za mazao, litakuwa msaada kwa wakulima wa eneo hilo.
Mandoo amesema baada ya kuona changamoto ya magari makubwa ya kubeba mizigo kufika eneo hilo kufuata mazao alijenga ghala hilo ili kurahisisha hali hiyo.
“Pamoja na kutumia mimi binafsi ghala hili pia wakulima wenzangu wataweza kuhifadhi mazao yao kwa lengo la kurahisisha uwekaji mazao katika eneo lenye usalama wa kutosha,” amesema Mandoo.
Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka huu wa 2025, Ismail Ussi amempongeza Mandoo kwa uwekezaji alioufanya wa ghala la mazao
Ussi amesema ghala hilo litawanufaisha wakulima kwa kuhifadhi mazao yao katika mahali sahihi na penye usalama na kuyaongeza thamani.
“Pia ghala hili litaongeza usalama wa chakula na ukusanyaji wa mazao katika eneo hili na kuongeza ajira kwa vijana na wanawake wa eneo hili la Mamire,” amesema Ussi.
Mkuu wa Wilaya ya Babati, Emmanuela Kaganda amempongeza mwekezaji Mandoo kwa kufanikisha ujenzi wa ghala hilo la kuhifadhi mazao mbalimbali.