Chuo Kikuu Mzumbe, kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Antwerp cha nchini Ubelgiji wamezindua rasmi mradi wa Kuwezesha mabadiliko chanya ya mila na desturi katika Kukabiliana na ndoa za utotoni nchini Tanzania (RE-EMPOWER) ambao umelenga kushughulikia changamoto za kijamii, kiuchumi na kimazingira ambazo zimebainika kuwa ni vichocheo vya ndoa za utotoni nchini Tanzania.
Uzinduzi wa Mradi huo umefanyika Agosti 14 katika ukumbi wa Maekani , Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi Kuu na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo Wataalamu wa ustawi wa jamii, wanataaluma, pamoja na viongozi wa dini na serikali, Kamishna wa Ustawi wa Jamii,
Akizungumza kwenye uzinduzi huo Kamishna wa Ustawi wa jamii Dkt. Nandera Mhando amesema kuwa ni muhimu kudumisha mila na desturi kwani ndizo zinastawisha jamii , lakini mradi huu unatoa fursa ya kushirikisha jamii katika kutatua changamoto za ndoa za utotoni wakati huo huo ukuendeleza mifumo bora ya kijamii
Aliongeza kuwa tafiti zinazofanywa ndani ya mradi huu zinatoa ushahidi wa kisayansi unaosaidia serikali na wadau kupanga sera na mikakati inayolenga matokeo halisi ya jamii na kuwasisitiza Wadau wote kushiriki vyema katika utafiti huo ili kupata majawabu sahihi ya changamoto ya ndoa za utotoni
Kwa upande wake Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Prof. Allen Mushi, alisisitiza kuwa mradi wa RE-EMPOWER unalingana na kauli mbiu ya chuo hicho inayosema “Tujifunze kwa Maendeleo ya Watu” kwa kuwa unalenga kutatua changamoto halisi kupitia tafiti zinazotoa maarifa na suluhisho chanya kwa sera na mikakati ya maendeleo.
Aidha Prof. Mushi alisisitiza kuendeleza ushirikiano kati ya Mzumbe, Chuo Kikuu cha Antwerp, na wadau wengine na kusema kuwa jambo hilo litaongeza ubora wa kitaaluma na kuimarisha nafasi ya chuo katika viwango vya kimataifa.
Awali, Dkt. Seraphina Bakta ambaye ni Mtiva wa Kitivo cha Sheria, alielezea kwa kina umuhimu wa mradi huu wa miaka mitano katika kushughulikia matatizo ya ndoa za utotoni yanayosababishwa na tabia na mazingira na kubainisha jinsi mradi huo ulivyolenga kutoa suluhisho na fursa kwa Wanataaluma kutoka chuo Kikuu cha Antwerp na Chuo kikuu Mzumbe kufanya tafiti zinazohusiana na ndoa za utotoni na masuala ya kijamii yanayohusiana na sheria.
Mratibu wa Mradi huo Dkt. Isabelle Zundel kutoka Chuo Kikuu cha Antwerp, alisema:
“Tunafurahia kushirikiana na Chuo Kikuu Mzumbe katika mradi huu unaolenga kutoa matokeo chanya katika kuzuia ndoa za utotoni. Mradi huu ni mfano wa jinsi elimu, utafiti na jamii vinaweza kuunganishwa kuleta mabadiliko yanayohitajika.”
Mradi wa RE-EMPOWER ni kielelezo cha jinsi ushirikiano kati ya vyuo vikuu, serikali, jamii na wadau wa kimataifa unavyoweza kuleta mabadiliko chanya ya kijamii. Kwa kushirikisha maarifa, tafiti na mila za kienyeji, mradi huu unatoa mwanga wa matumaini kwa vijana, unasaidia kupunguza ndoa za utotoni, na unaweka msingi wa jamii yenye afya, elimu bora, na usawa wa kijinsia.







Baadhi ya wahadhiri wa chuo kikuu mzumbe na wadau mbalimbali wa nje walioshirikiuzinduzi wa mradi wa RE – EMPOWER