Ofisa Habari wa Yanga SC, Ali Kamwe, amesema usajili wa wachezaji wakubwa ndani ya klabu hiyo ni sehemu ya mpango wa kujenga kikosi imara kuelekea msimu wa 2025/26.
Kamwe alibainisha kuwa Yanga, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara msimu wa 2024/25 waliomaliza na pointi 82 na mabao 83, wanajiandaa kushindana katika Ligi Kuu na Ligi ya Mabingwa Afrika.
“Unaona saini ya Mohamed Hussen Zimbwe Jr namna ambavyo imekuwa gumzo kila kona. Hii inaonyesha tunafanya usajili mkubwa kwa ajili ya mashindano makubwa tunayoshiriki,” alisema Kamwe.
Aliongeza kuwa ili Yanga iwe mshindani katika ngazi ya ndani na kimataifa, ni lazima kujenga kikosi chenye wachezaji wenye ubora wa hali ya juu.