Mkuu wa Wilaya ya Kasulu,mkoani Kigoma, Mhe. Kanali Isaac Mwakisu, amesema wananchi wanapaswa kujitokeza kwa wingi kushiriki mapokezi ya Mwenge wa Uhuru pamoja na Uchaguzi Mkuu ujao, kwani matukio hayo ni ya kitaifa na yanabeba taswira ya mshikamano wa Watanzania.

Baadhi ya viongozi na wananchi waliojitokeza kwenye bonanza hilo
Mkuu wa Wilaya ya Kasulu,mkoani Kigoma, Mhe. Kanali Isaac Mwakisu na katibu tawala Theresia Mtewele wakishiriki katika bonanza kwa ajili ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru pamoja pamoja na kuhamasishwa wananchi kushiriki Uchaguzi Mkuu ujao,
Na Fredy Mgunda, Kigoma.
MKUU wa Wilaya ya Kasulu,mkoani Kigoma, Mhe. Kanali Isaac Mwakisu, amesema wananchi wanapaswa kujitokeza kwa wingi kushiriki mapokezi ya Mwenge wa Uhuru pamoja na Uchaguzi Mkuu ujao, kwani matukio hayo ni ya kitaifa na yanabeba taswira ya mshikamano wa Watanzania.
Akizungumza leo Jumamosi, Septemba 6, 2025, katika bonanza la michezo mbalimbali lililofanyika Viwanja vya Shule ya Msingi Kiganamo, Kanali Mwakisu amesema Mwenge wa Uhuru utakimbizwa wilayani humo Septemba 17 na 18, ambapo siku ya kwanza utapokelewa Kasulu Vijijini eneo la Mvugwe na siku inayofuata itakuwa Kasulu Mjini.
“Maudhui makuu ya bonanza hili ni kuwakumbusha wananchi kuwa Mwenge utakimbizwa katika wilaya yetu, na tunapaswa kushiriki kwa wingi ili kuonesha mshikamano na kuthamini amani na utulivu wa nchi yetu,” amesema.
Amesema kuwa Mwenge wa Uhuru ni tunu kubwa ya taifa, na wananchi wanapojitokeza kuupokea kwa shangwe ni kielelezo cha kuthamini amani na utulivu kwa mustakabali wa maendeleo ya nchi.
Aidha, amewakumbusha kuwa kwa mujibu wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Uchaguzi Mkuu utafanyika Oktoba 29, 2025, hivyo wananchi wanatakiwa kujitokeza kwa wingi baada ya kusikiliza sera za wagombea na kuwachagua viongozi wanaowataka.
Mmoja wa wananchi, Nelstella Kihoza, akizungumza na mwandishi wetu amesema kuwa umati mkubwa uliofurika viwanjani hapo ni ishara tosha ya mwamko wa wananchi wa Kasulu, na kwamba watajitokeza kwa wingi kushiriki Uchaguzi Mkuu kwa kuchagua viongozi wanaowataka, sambamba na kushiriki kikamilifu katika Mbio za Mwenge wa Uhuru.
Naye Mwalimu Yusufu Hamisi amrmpongeza Mkuu wa Wilaya kwa ubunifu wa kuandaa bonanza hilo, akisema limempa ari ya kuendelea kuhamasisha wananchi wengine kushiriki kikamilifu matukio hayo mawili muhimu ya kitaifa.