Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Lindi
MGOMBEA urais kupitia Chama Cha Mapinduzi(CCM) Rais Dk.Samia Suluhu Hassan amewapongeza wananchi wa Wilaya ya Ruangwa wakiongozwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa kuwa na Uwanja wa mpira mkubwa na wa kisasa.
Dk.Samia ametoa pongezi hizo leo Septemba 24,2025 alipokuwa katika mkutano wa kampeni uliofanyika Uwanja wa Madini wilayani Lindi ambapo maelfu ya wananchi wa Wilaya hiyo wamejitokeza kwa wingi.
“Niwapongeze wananchi wa wilaya ya Ruangwa kwa kupata uwanja mzuri wa michezo wa Majaliwa ambao ni chachu ya maendeleo kwa vijana na kuinua vipaji.
“Uwanja huu umechangia kuibua vipaji vya soka nchini ikiwemo Timu ya Namungo inayoshiriki Ligi Kuu ya Soka ya NBC.Naamini uwepo wa Uwanja huu tutaendelea kushuhudia vipaji zaidi vya wachezaji soka vikiibuka.”
Dk.Samia amesema pia CCM inaamini michezo ni fursa nyingine ya ajira, ajira ya kuajiriwa na ajira binafsi. “Serikali yetu imetoa kipaumbele kuunga mkono jitihada hizo.
“Natambua michezo ni furaha, kutambuana, kujengeana imani kwa hiyo nikupongeze sana Majaliwa kwa kujenga uwanja huo na kuifanya Ruangwa iwe na sehemu nzuri ya michezo,” amesema.
Akieleza kuhusu michezo amesema anafahamu hata wakiwa katika Baraza la Makamu wa Rais Dk.Philip Mpango ni shabiki wa Yanga na Mawaziri Mkuu Mkuu Kassim Majaliwa ni shabiki wa Simba,wanataniana lakini michezo ni furaha.Tunakupongeza Waziri Mkuu kwa Uwanja huu.”