Serikali Watoa Maelezo Kwanini Pamba Jiji Walifanya Mazoezi Kukiwa na Giza Kwa Mkapa
Serikali kupitia Wizara ya sanaa, utamaduni na michezo umetoa ufafanuzi kuhusiana na tukio la wachezaji wa Pamba Jiji kufanya mazoezi gizani ugani Benjamin Mkapa .
“Kufuatia taarifa inayosambaa mitandaoni ikionesha wachezaji wa timu ya Pamba Jiji FC wakifanya mazoezi gizani katika uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo inapenda kuufahamisha umma kuwa timu hiyo ilifika katika uwanja huo bila taarifa rasmi ya kuja kufanya mazoezi ya kujiandaa na mchezo wao dhidi ya timu ya Yanga SC hapo kesho tarehe 24 Septemba, 2025.
“Kwa kuwa Timu haikuwa imetoa taarifa mapema, baada ya kuwasili katika uwanja huo majira ya saa 12:35 jioni wataalamu wa umeme uwanjani hapo walikuwa wameishaondoka, hivyo ikalazimu kuwarudisha kazini na kufanikiwa kuwasha taa za uwanja huo saa 1:08 usiku.
“Wizara imesikitishwa na usambazaji wa picha jongevu zinazoonesha wachezaji wakifanya mazoezi gizani licha ya kuwa chanzo chake ni makosa ya timu ya Pamba Jiji FC yenyewe na imekiona kitendo hicho kama ni kuharibu heshima na taswira ya menejimenti ya uwanja ambayo imekuwa ikifanya kazi kuzingatia taratibu zilizowekwa Wizara inazitaka timu za mpira wa miguu zilizoomba kutumia uwanja wa Benjamin Mkapa kwa mashindano mbalimbali kuzingatia taratibu za matumzi ya uwanja huo ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa mapema pindi timu zinapotaka kufanya mazoezi ya mwisho kabla ya mechi ili maandalizi muhimu yafanyike badala ya kuja ghafla na kusababisha sintofahamu isiyo lazima.”. Barua hiyo ilieleza.