MSHAMBULIAJI mpya wa Yanga SC, Buba Jammeh, ameeleza furaha yake kubwa baada ya kuona mashabiki wakiimba jina lake, akiamini kuwa uhamasishaji huo utaendelea kumpa nguvu kuwaletea matokeo mazuri klabuni.
Amesema kuwa hamasa aliyopewa na wapenzi wa Yanga imemfanya ajitahidi zaidi uwanjani, akilenga kulinda heshima ya jina lake na nembo ya klabu kwa kushirikiana na wenzake.
Buba, aliyejisajili mwishoni mwa dirisha dogo la usajili, anatarajia kuonekana Jumapili katika mechi ya mwisho ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya JS Kabylie, ambapo atakuwa sehemu ya kikosi cha kwanza.
“Nimefurahi kuwa sehemu ya kikosi cha timu ya Yanga. Jumapili itakuwa mechi yangu ya kwanza tangu kutua hapa. Yanga ni timu kubwa na niko hapa kupambana ili kufikia malengo ya timu,” amesema Buba.
Kuhusu mchezaji aliyemvutia kujiunga na Yanga, Buba ameeleza kuwa Stephane Aziz Ki, aliyewahi kuvaa jezi namba 10, ndiye aliyechangia sana katika uamuzi wake kuhamia klabu hiyo.
Mashabiki wa Yanga wanashangilia nafasi ya kumwona mshambuliaji huyo akiwakilisha timu katika mchezo wa Jumapili, utakaochezwa kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, visiwani Zanzibar, na wanatarajiwa kuipa timu hamasa kubwa uwanjani.
The post BUBA PULIZA MOTO YANGA, JINA LAKIMBIWA appeared first on Soka La Bongo.



