KOCHA wa Stade Malien, Mauril Njoya, amekiri kushangazwa na mwenendo wa Kundi D la Ligi ya Mabingwa Afrika, akisema hakutarajia kuona timu yake ikiongoza kundi hilo mbele ya Simba SC katika hatua hii ya mashindano.
Akizungumza kuelekea mchezo wa mwisho wa kundi hilo utakaopigwa kesho kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Njoya amesema matarajio yake kabla ya kuanza kwa michuano hiyo yalikuwa tofauti kabisa na hali ilivyo sasa.
Kocha huyo alieleza kuwa aliiheshimu Simba kama moja ya timu kubwa na zenye uzoefu mkubwa barani Afrika, hivyo aliamini wangetamalaki kundi hilo huku Stade Malien wakimaliza katika nafasi ya pili nyuma ya Wekundu wa Msimbazi.
Katika msimamo wa sasa wa Kundi D, Stade Malien wamefanikiwa kukata tiketi ya robo fainali wakiwa vinara, wakiwaacha nyuma vigogo kama Espérance Sportive de Tunis na Petro de Luanda, huku Simba wakishika mkia wa kundi hilo.
Hali hiyo imeibua mshangao kwa wengi, akiwemo Njoya mwenyewe ambaye hakusita kuweka wazi hisia zake.
“Simba ni moja ya timu bora sana Afrika, sijui imekuwaje tupo juu yao. Kiukweli nilitarajia Simba kumaliza nafasi ya kwanza na sisi kuwa nafasi ya pili,” amesema Njoya.
Pamoja na mshangao huo, kocha huyo amesisitiza kuwa kikosi chake kimejipanga vyema kwa ajili ya mchezo wa kesho, akiahidi kupambana kuhakikisha wanamaliza hatua ya makundi kwa ushindi.
Ameongeza kuwa licha ya Simba kutokuwa na matokeo mazuri msimu huu, bado ni timu yenye heshima kubwa barani Afrika, hivyo wataingia uwanjani kwa tahadhari kubwa wakitambua ubora na uzoefu wa wapinzani wao katika michuano ya kimataifa.
The post SIMBA YAMUACHA MDOMO WAZI KOCHA STADE MALIEN appeared first on Soka La Bongo.


