Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Mhe. Dkt. Tulia Ackson, leo tarehe 10 Aprili 2025, amekutana na kufanya mazungumzo na Meya wa Jiji la Tashkent nchini Uzbekistan, Mhe. Shavkat Umurzakov Buranovich, katika Ofisi za Meya huyo zilizopo katika Jiji hilo.
Katika mazungumzo hayo, Viongozi hao wamejadili njia bora za kuimarisha ushirikiano na mahusiano kati ya Tanzania na Uzbekistan katika sekta mbalimbali ikiwemo diplomasia, utalii, afya, elimu pamoja na kuanzisha uhusiano wa kimaendeleo baina ya Jiji la Mbeya na Jiji la Tashkent.
Dkt. Tulia aliambatana na Ndg. Joshua Magigita, Mwakilishi wa Balozi wa Tanzania nchini Urusi ambaye pia anahudumia nchi ya Uzbekistan.
Kwa upande wake, Meya wa Tashkent ameonesha nia thabiti ya kuendeleza mashirikiano hayo kwa haraka, na ameeleza kuwa anatarajia kufanya ziara ya kutembelea Tanzania katika siku zijazo.