Julieth Kabyemela
Na Rose Ngunangwa, Dar es Salaam
Serikali imesisitiza umuhimu wa kulinda lugha za asili kwani ni nyenzo ya utu ya utamaduni usioshikika.
Wito huu ulitolewa jana na Mkurugenzi Msaidizi wa Utamaduni kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Julieth Kabyemela wakati akifungua kikao kazi cha wanufaika wa ruzuku ya pili ya Mradi wa UNESCO- Alwaleed Philanthropies.
Alisema uanuai wa lugha ni rasilimali ya thamani sana barani Afrika kwani imechangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa lugha ya Kiswahili.
“Tunahitaji kuendeleza jitihada za kuhakikisha kuwa kunakuwa na jamii jumuishi na anuai ya kiutamaduni ili kulinda tunu, maadili na urithi wa kiutamaduni,” alisema Kabyemela.
Kwa upande wake, Mkuu wa Ofisi ya UNESCO bwana Michel Toto amesema kuwa mradi huo unalenga kutoa msaada wa kifedha na kiufundi kwa wanufaika 10 ili kuleta matokeo ya kudumu katika jamii wanazofanyia kazi kwa kutumia utamaduni na elimu ili kutengeneza fursa za kiuchumi kwa vijana na wanawake.
“ Mradi huu unalenga kuhifadhi utajiri wa urithi wa utamaduni Tanzania na kukuza ujuzi wa maswala ya utamaduni na kujenga uendelevu wa maisha,” alisema bwana Toto.
Mashirika matano yaliyopata ruzuku hiyo kwa awamu ya pili ya Mradi wa UNESCO- Alwaleed Philanthropies ni CCBRT (Dar es Salaam), EYP ( Mbeya), DCMA ( Zanzibar) ATAFO ( Arusha) and CDEA ( Dar es Salaam).
Mkuu wa Ofisi ya UNESCO bwana Michel Toto akizungumza
Wawakilishi wa Mashirika yaliyopata ruzuku kwa awamu ya pili