NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, amesema kuwa serikali itaendelea kushirikiana na wawekezaji na kudumisha mashirikiano yenye tija kwa maendeleo ya taifa.
Akizungumza Mei 26, 2025 jijini Dar es Salaam wakati wa ziara ya kampuni ya Puma Energy katika ofisi za Hazina, Mchechu alieleza kuwa kampuni hiyo inamilikiwa kwa asilimia 50 na Serikali ya Tanzania, huku asilimia nyingine 50 ikimilikiwa na wawekezaji binafsi.
Alisisitiza kuwa ushirikiano huo wa kimkakati ni muhimu kwa maendeleo ya sekta ya nishati nchini.
“Tutaendelea kufanya mageuzi na kuboresha matumizi ya rasilimali zetu ili kuhakikisha Taifa linanufaika kwa kiwango cha juu. Tunataka kuona kampuni kama Puma Energy zikizalisha faida na mapato mara mbili zaidi kupitia matumizi bora ya nishati.”alisema Mchechu.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy duniani, Marc Russel, alieleza furaha yake kuwa sehemu ya uwekezaji barani Afrika, hususan nchini Tanzania, akibainisha kuwa ni eneo lenye fursa nyingi za kiuchumi na biashara.
Naye Mkurugenzi wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah, alisema Tanzania inaongoza kwa mapato na faida kati ya nchi zinazohudumiwa na Puma, na kuitaja kuwa ni nchi ya kimkakati kwa mustakabali wa kampuni hiyo.
“Tuna dhamira ya kuimarisha zaidi ushirikiano wetu na Serikali ya Tanzania ili kukuza uchumi na kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi,” alisema Fatma.