WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,Mhe
George Simbachawene,akziungumza wakati akifungua Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.

……
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene, ametoa wito kwa taasisi zote za umma ambazo bado hazijajiunga na Mfumo wa Serikali wa Mawasiliano ya Ndani (GovESB) kuhakikisha zinafanya hivyo haraka ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.
Akizungumza leo Juni 17,2025 wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, Waziri Simbachawene amesema kuwa hadi sasa ni taasisi 185 pekee ndizo ambazo tayari zimeunganishwa kwenye mfumo huo unaowezesha huduma kutolewa kwa urahisi na kwa pamoja, hivyo kupunguza adha kwa wananchi.
“Taasisi ambazo bado hazijajiunga, zichukue hatua mara moja. Mfumo huu umeletwa kwa nia njema ya kurahisisha huduma na kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma bila kulazimika kufuata ofisi mbalimbali,”amesema Simbachawene
Kwa mujibu wa Waziri huyo, mfumo huo unahakikisha kuwa huduma za serikali zinaingiliana (interoperability) na kurahisisha wananchi kupata huduma kwenye kituo kimoja badala ya kuhangaika katika taasisi nyingi, hali inayookoa muda na gharama.
Hata hivyo Simbachawene amesema kuwa wiki ya utumishi wa imma inalenga kuonyesha mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa, sambamba na kuwapa hamasa ya kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uaminifu mkubwa.
“Wiki hii ni jukwaa muhimu kwa wananchi kuelewa haki na wajibu wao, lakini pia taasisi za serikali hupata nafasi ya kupokea mrejesho kutoka kwa wadau na wananchi ili kuboresha huduma,” ameeleza
Aidha, amezitaka taasisi ambazo hazijashiriki maadhimisho hayo mwaka huu kujipanga kushiriki miaka ijayo kwa kuwa ni fursa ya pekee ya kukutana uso kwa uso na wateja wao na kusikia maoni yao.