:::::::::
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAKRISTO nchini wameaswa kuwa waangalifu dhidi ya mafundisho yenye upotoshaji wanapokuwa katika nyumba za ibada, hali inayoweza kusababisha migongano baina yao na hatimaye kuvuruga amani katika jamii.
Rai hiyo imetolewa na Askofu Dk. Batolomeo Sheggah, wakati wa ibada ya kumsimika Askofu Bahati Nyagawa kuwa Askofu Mkuu wa Makanisa ya Devine Healing Assemblies Church (DHAC), ibada iliyofanyika katika kanisa la DHAC lililopo Ulongoni, Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam.
Dk. Sheggah alisema mafundisho yenye kupotosha yameendelea kuingia makanisani na kusababisha mkanganyiko kwa waumini, jambo ambalo linahitaji tahadhari kubwa.
“Ni muhimu kwa waumini kujifunza neno la Mungu kwa usahihi na kuchambua mafundisho wanayopewa ili kuepuka kuingia katika mitego ya kiroho inayoweza kuwapeleka mbali na ukweli,” alisema Dk. Sheggah.
Kwa upande wake, Askofu Bahati Nyagawa alisema mahubiri yao yanalenga kuifundisha jamii kuishi kwa kweli na kumtegemea Mungu, hali ambayo itasaidia kuunda jamii yenye uadilifu.
“Tumeazimia kuhubiri kweli ili watu waweze kumjua Mungu na kuwa huru kutoka kwenye utawala wa kishetani,” alisema Askofu Nyagawa.
Aidha, Dk. Sheggah ambaye pia ni Askofu Mkuu wa Makanisa ya FPTC, aliongeza kuwa hatua ya Askofu Nyagawa kuitikia wito wa kiroho ni chachu na mfano wa kuigwa kwa viongozi wa dini nchini.
“Umekuwa Askofu sasa, utaliambia pepo toka litatoka; utasema mgonjwa pona, na atapona,” alisema Dk. Sheggah.
Naye Katibu Mkuu wa DHAC, Tumaini Jinathan, alisema kumsimika kwa Askofu Nyagawa ni hatua muhimu katika kuimarisha na kupanua huduma ya kiroho ya kanisa hilo ndani na nje ya nchi.
“Hatua hii ni mwanzo mzuri wa kuona DHAC ikikua na kutambulika zaidi katika kutoa huduma ya kiroho kwa jamii,” alisema Jinathan.
Katika hatua nyingine, mke wa Askofu huyo ambaye pia ni Mchungaji, Pendo Nyagawa, alisema atakuwa bega kwa bega na mumewe kuhakikisha anafanikiwa katika kueneza Neno la Mungu.
“Nitahakikisha namuombea kila siku na kumsapoti kwa kila hali na mali katika jukumu hili kubwa alilokabidhiwa na Mungu,” alisema Mchungaji Pendo.
Ibada hiyo ilihudhuriwa na waumini kutoka maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam na viongozi wa makanisa mengine, waliokuja kushuhudia tukio hilo la kihistoria katika kanisa hilo.