Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb), akijibu swali la Mheshimiwa Zahor Mohammed Haji (Mwera), aliyetaka kujua faida na hasara ya Tanzania kutokana na msimamo wa nchi za BRICS ambazo zimejipanga kujiondoa kwenye Mfumo wa Dolarisation, bungeni jijini Dodoma.
(Picha na Kitengo cha Mawasilino Serikalini, Wizara ya Fedha)
Na. Saidina Msangi, WF, Dodoma.
Serikali imesema kuwa Tanzania haitapata athari za moja kwa moja kutokana na mafanikio au changamoto zozote katika Umoja wa BRICS (Brazil, Russia, India, China na Afrika Kusini), zinazoweza kutokea katika sekta ya kiuchumi na fedha hususani ya kujiondoa kwenye Dolarisation kwa kuwa sio nchi mwanachama wa BRICS.
Hayo yalisemwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mheshimiwa Zahor Mohammed Haji (Mwera), aliyeuliza faida na hasara ya Tanzania kutokana na msimamo wa nchi za BRICS ambazo zimejipanga kujiondoa kwenye mfumo wa Dolarisation.
Alisema Serikali ya Tanzania imekuwa na ushirikiano wa muda mrefu na nchi za BRICS (Brazil, Russia, India, China na Afrika Kusini) katika nyanja mbalimbali ikijumuisha masuala ya kiuchumi, biashara na diplomasia kwa kuendelea kuwepo kwa balozi za nchi hizo hapa nchini na Tanzania kuwa na balozi katika nchi hizo.
’’Kwa sasa Tanzania sio mwanachama wa BRICS ila inashiriki katika mikutano ya BRICS kama observer, hivyo mafanikio au changamoto zozote katika umoja huo zinazoweza kutokea katika sekta ya kiuchumi na fedha hususani ya kujiondoa kwenye Dolarisation, hatutakuwa na athari za moja kwa moja kwa kuwa sio wanachama wa BRICS,’’ alifafanua Mhe. Chande.
Mhe. Chande alisema mahusiano ya Tanzania na nchi hizo yanadumishwa kwa kuendelea kuwepo kwa balozi za nchi hizo hapa nchini na Tanzania kuwa na balozi katika nchi hizo.
Aliongeza kuwa mahusiano hayo yanaendelea kuleta mafanikio chanya kwa Serikali ya Tanzania kwa kutumia fursa za kiuchumi zinazopatikana katika nchi hizo ambazo pia zinaimarisha mahusiano ya uwili baina yake (bilateral engagement).