Mbunge wa Dodoma Mjini na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde,akikata utepe kuashiria uzinduzi wa jengo la kupumzikia ndugu wa wagonjwa wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma hafla iliyofanyika leo Juni 25,2025 jijini Dodoma.
Na Alex Sonna, Dodoma
Mbunge wa Dodoma Mjini na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, ameonyesha furaha yake kubwa baada ya kutimiza ahadi na ndoto yake ya muda mrefu ya kujenga jengo la kupumzikia ndugu wa wagonjwa wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa jengo hilo, Leo Juni 25,2025 Mavunde alisema kuwa dhamira hiyo aliiweka tangu akiwa mgombea ubunge kwa mara ya kwanza mwaka 2010, ingawa hakufanikiwa wakati huo.
Ameeleza kuwa alitamani sana kupata nafasi ya uongozi katika eneo alilozaliwa ili aweze kuchangia maendeleo na kusaidia wananchi kwa dhati
Mavunde amesema kuwa alipochaguliwa kwa mara ya kwanza mwaka 2015 aliahidi kwa wanachi kuwa mtumishi wa watu badala ya kuwa kiongozi wa kawaida.
“Mwaka 2017 nilianzisha mfumo wa kidijitali kuhakikisha kuwa watumishi wanafika kazini kwa wakati na kuwatendea wagonjwa kwa heshima,nilifunga kamera na maikrofoni katika eneo la huduma za wagonjwa wa nje ili kuimarisha uwajibikaji na kuhakikisha wagonjwa wanapata huduma bora, “ameeleza
Mbunge huyo pia alikumbushia tukio la siku moja alipofika usiku hospitalini akiwa ameambatana na mgonjwa na kukuta wananchi wengi wamelala nje ya geti wakichanganyika bila kujali jinsia jambo lililomuumiza na kushawishika kuwajengea mahala pazuri.
Amesema hali hiyo ilimuumiza sana na kumfanya aazimie kujenga jengo la kupumzikia ili kuwasaidia wananchi hao. Jengo hilo lina mabenchi 24 ya kukalia, televisheni kwa ajili ya kutoa taarifa muhimu na uzio kwa ajili ya usalama.
“Asilimia kubwa ya watu waliokuwa wakikaa nje ya hospitali siyo wakazi wa Dodoma bali ni watu wanaosafiri kutoka mikoa mingine, hivyo moyo wake ulimsukuma kuwajengea sehemu hiyo kama mchango wake kwa jamii,” Amesema Waziri Mavunde.
Hata hivgo ametoa ombi maalum kwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kuangalia kwa jicho la huruma akinamama wanaouza vyakula katika eneo hilo kwa kuwapa nafasi rasmi ya kufanya biashara, huku akiahidi kuwaletea eneo lenye kivuli ili wafanye kazi zao katika mazingira bora
Katika hatua nyingine, Mavunde ametoa shukrani kwa wadau waliomsaidia kutimiza ndoto hiyo akiwemo Mkurugenzi wa Asasi ya Salim Asasi, mchezaji wa Yanga Aziz Ki , Golikipa wa Yanga Djigui Diarra pamoja na mfanyabiashara Vencampan ambao walichangia asilimia 80 ya gharama za ujenzi wa jengo hilo
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemery Senyamule ambaye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo alisema jengo hilo ni tumaini jipya kwa wananchi na litaleta faraja kwa wale wanaouguza ndugu zao hospitalini.
Amempongeza Mavunde kwa moyo wake wa huruma na kwa kutimiza kwa vitendo ahadi alizozitoa
Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma Dkt Ibenzi Ernest alisema kuwa dira ya hospitali hiyo ni kutoa huduma bora kwa wananchi na kwamba mchango wa Mbunge Mavunde umekuwa wa thamani kubwa kwa maendeleo ya hospitali hiyo.
Alisema licha ya changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa watumishi na uzio wa hospitali bado hatua kama hizi zinaonyesha jitihada za kweli katika kuboresha huduma kwa wananchi wa Dodoma na wageni wanaofika .







