Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (INEC),Jaji wa Mahakama ya Rufani Jacobs Mwambegele,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa ratiba rasmi ya uchaguzi Mkuu 2025 iliyofanyika leo Julai 26,2025 jijini Dodoma
Na.Alex Sonna-DODOMA
TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imesema kuwa Kampeni kwa ajili ya uchaguzi Mkuu 2025 kwa kuwachagua Madiwani,wabunge pamoja na Rais,zinatarajiwa kuanza rasmi Agosti 28,mwaka huu.
Hayo yamebainishwa leo Julai 26,2025 jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi,Jaji wa Mahakama ya Rufani Jacobs Mwambegele,katika hafla ya uzinduzi wa ratiba rasmi ya uchaguzi Mkuu 2025.
Jaji Mwambegele,amesema kuwa vituo 99,911 vitatumika kwa ajili ya kupiga kura kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Kwa mchanganuo ufuatao vituo 97,349 vitatumika kwa ajili ya kupiga kura kwa upande wa Tanzania bara na vituo 2562 vitatumika kwa ajili ya Tanzania Zanzibar”amesema Jaji Mwambegele
Amesema kuwa idadi hiyo ya vituo 99,911 ni sawa na ongezeko la asilimia 22.49 ya vituo vya kupigia kura 81467 vilivyotumika katika uchaguzi Mkuu 2020.
Aidha amesema kuwa baada ya uchakataji wa taarifa za uchaguzi kukamilika,Tume imebaini kuwa jumla ya wapiga kura wapya 7,641,592 wameandikishwa katika Daftari la kudumu la wapiga kura ,sawa na asilimia 136.79 ya madirio ya awali.
“Jumla ya wapiga kura 4,291,699 wameboresha taarifa zao,sawa na asilimia 98.23 ya makadirio ya awali huku wapiga kura 99,744 wakiwekwa nje ya daftari kwa kupoteza sifa,idadi inayolingana na asilimia 16.78 ya makadirio ya awali”amesema
Aidha amesema wapiga kura 8,703 wamebainika kujiandikisha zaidi ya mara moja,kinyume na sheria na taratibu za uandikishaji,kitu ambacho ni kosa la jinai.