

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango, ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-Organ Troika Summit) kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mkutano huo umefanyika kwa njia ya mtandao huku Dkt. Mpango akishiriki akiwa Babati mkoani Manyara.
Mkutano huo umeongozwa na Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC, ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Malawi, Mheshimiwa Prof. Arthur Peter Mutharika.
Viongozi wa SADC wamejadili kwa kina hali ya kisiasa na usalama katika Jamhuri ya Madagascar kufuatia mapinduzi ya kijeshi yaliyotokea hivi karibuni nchini humo.
Kupitia majadiliano hayo, Mkutano umeeleza dhamira ya dhati ya nchi wanachama wa SADC kuunga mkono juhudi za kurejesha amani, utulivu na utawala wa sheria nchini Madagascar.
Aidha, viongozi hao wametoa wito kwa wananchi wa Madagascar kuhakikisha wanatumia njia ya mazungumzo kutatua changamoto zilizopo, na kuepuka vitendo vya vurugu, uporaji na uharibifu wa mali ambavyo vinaweza kuhatarisha mustakabali wa taifa hilo.
Mkutano pia umeiagiza Sekretarieti ya SADC kushirikiana kwa karibu na Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU), pamoja na Kamisheni ya Nchi za Bahari ya Hindi (IOC) ili kuhakikisha uratibu wa pamoja katika jitihada za kutafuta suluhu ya kudumu ya mgogoro wa Madagascar.
MIILI ya VIJANA 4 YAOKOTWA PWANI IKIWA na MAJERAHA – YUPO wa MIAKA 19 na 21 – KAMANDA AELEZA…