UONGOZI wa klabu ya Yanga umefikia makubaliano ya kubadilishana wachezaji na klabu ya Singida Black Stars katika mpango unaolenga kuimarisha vikosi vya pande zote mbili kuelekea michuano ijayo.
Kupitia makubaliano hayo, kiungo mkabaji wa Singida Black Stars, Mohamed Damaro Camara, anatarajiwa kutua Yanga, huku beki Balla Conte akielekea kujiunga na Singida Black Stars maarufu kama Walima Alizeti.
Taarifa zinaeleza kuwa mazungumzo kati ya klabu hizo mbili yamekamilika kwa mafanikio, ambapo kila upande umeridhia masharti ya makubaliano yaliyowekwa mezani.
Aidha, Camara ambaye ni raia wa Guinea, tayari amekubali kujiunga na Yanga baada ya kuvutiwa na mradi wa klabu hiyo pamoja na nafasi ya kucheza michuano mikubwa ya ndani na kimataifa.
Kwa mujibu wa vyanzo vya karibu na klabu, Yanga inatarajiwa kukamilisha taratibu zote za usajili muda wowote kuanzia sasa ili kumruhusu Camara kuanza mazoezi na kikosi mara moja.
Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mkakati wa Yanga kuimarisha safu ya kiungo mkabaji, huku Singida Black Stars nayo ikitarajia kunufaika na ujio wa Balla Conte katika kuimarisha safu ya ulinzi wa timu hiyo.
The post CAMARA NDANI YA JANGWANI, BALLA KONTE SINGIDA appeared first on Soka La Bongo.








