Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu wamehimizwa kuratibu vyema taarifa za utekelezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita na kuzisemea kazi hizo kwa wananchi ilia wapate uelewa wa uhakika wa miradi ya maendeleo iliyofanywa na Serikali katika maeneo yao.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uaratibu) Mheshimiwa William Lukuvi wakati akifungua kikao cha baraza la wafanyakazi la Ofisi ya Waziri Mkuu, katika Ukumbi wa Ngome Jijini Dodoma leo tarehe 14 Machi, 2025.
Ameongeza kusema Watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu wana majukumu makubwa hivyo wanapaswa kuwa kioo katika utekelezaji wa kazi vizuri na usimamizi wa shughuli za Serikali ili waweze kuratibu taarifa za mafanikio kwa wananchi.
“Tunalo jukumu la kuwaambia wananchi kazi zilizofanywa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi chake cha uongozi na kwa kuzipambanua vizuri ikiwa ni sehemu ya uratibu ili wananchi wazijue kwa uhakika huko waliko,” alieleza Waziri.
Ili tuweze kuratibu lazima majukumu yaliyo ndani ya Ofisi yetu yaweze kusimamiwa vizuri sana kwa kuwa mfano katika idara zetu ili tuweze kusimamia idara na taasisi zilizo nje vizuri.
Amefafanua, Waziri Mkuu anaamini kwamba watendaji wa Ofisi yake wapo na wanamsaidia katika jukumu kubwa la kuratibu shughuli zote za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Nikupongeze tena Katibu Mkuu Dkt. Yonazi kwa usimamizi mzuri na timu ya menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tuendele kushirikiana katika kufanya kazi lakini niwapongeze Wakuu wa Idara na Vitengo nimewatembelea mnafanya vizuri sana,” alisema Waziri.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi ameshukuru Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Naibu Waziri wa Ofisi hiyo kwa miongozo mizuri wanayotoa ili kuweza kutimiza majukumu ya kila siku.
“Viongozi wetu Wakuu wanafahamu kazi ambazo tumekuwa kukizifanya na kwa kupitia nyie tunaomba mtufikishie salamu za shukrani kwao,”
Naye Msaidizi wa Katibu wa (TUGHE) Mkoa wa Dodoma Maisha Mbilla amesema wanafahamu kwamba watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) wanafanya kazi kwenye mazingira mazuri na wanapata stahiki zao vizuri, na kuupongeza uongozi wa Ofisi hiyo.
“Hii inatutia faraja na moyo na tuna wajibu kama Chama Cha Wafanyakazi wakuongea na watumishi ili waendelee kufanya kazi kwa kufuata sheria kanuni na taratibu pamoja na miongozo ya Utumishi wa Umma,”