Na Mariam Mkamba, Tabora
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Tanzania Bara Stephen Wasira amewaahidi wakulima wa tambaku mkoani Tabora kuwa fedha zao za ruzuku Sh.bilioni 13 wanazodai kwa muda mrefu watalipwa mwishoni mwa Aprili mwaka huu.
Wasira ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Tabora akihitimisha ziara yake ya kikazi katika Mkoa huo ambapo amesema moja ya changamoto aliyokutana nayo ni madai ya fedha za ruzuku za wakulima wa tumbaku ambazo wanadai kwa muda mrefu.
“Serikali imetenga Shilingi bilioni 13 kwa ajili ya kuwalipa wakulima wa tumbaku na asilimia 70 ya fedha hizo zitaelekezwa Tabora.Niliahidi wananchi kuwa nitazungumza na wahusika kuhusu kero ya malipo ya wakulima wa tumbaku, leo nimepata majibu kuwa ruzuku yao italipwa kabla ya mwezi huu kuisha,” amesema Wasira.
Amefafanua ucheleweshaji wa malipo hayo ulitokana na zoezi la uhakiki baada ya baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika kuongeza majina ya watu ambao hawakulima tumbaku kwenye orodha ya walengwa wa malipo, hali iliyosababisha sintofahamu na kuchelewesha mchakato.
“Vyama vya ushirika waliambiwa waseme nani ameuza nini, lakini wakaanza kuongeza watu wasiostahili. Serikali ililazimika kuhakiki upya majina yote, na sasa kazi hiyo inakaribia kukamilika,” ameongeza.
Wakulima wa tumbaku wamekuwa wakilalamikia ucheleweshaji wa malipo kwa muda mrefu, hali iliyozua changamoto katika maandalizi ya msimu mpya wa kilimo pamoja na maisha yao ya kila siku.
Wasira amesema serikali ya CCM itaendelea kusimamia maslahi ya wakulima ili kuhakikisha wanapata haki zao kwa wakati, huku akiwataka viongozi wa ushirika kuwa waaminifu kwa wakulima.