Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
MWANZILISHI Mwenza wa Shirikisho la Wanasayansi Chipukizi (YST) Dk. Gozibert Kamugisha amesema mwaka huu Shirikisho hilo limepokea idadi kubwa ya maombi ya kazi za kisayansi kutoka kwa wanafunzi wanaomba kushiriki mashindano hayo.
Dk.Kamugisha amesema kwamba maombi hayo ni ongezeko la asilimia 43 kwa idadi ya kazi za kisayansi zilizowasilishwa mwaka 2025 ikilinganishwa na maombi 1,055 mwaka 2024.
Dk.Kamugisha amesema mashindano hayo yatafanyika Septemba 18, 2025 na kufafanua kutoka na idadi hiyo inamaanisha wanafunzi 3,032 wameshiriki kutuma maombi kwa kuwa ombi moja la kazi ya sayansi linawasilishwa kwa ushirikiano wa wanafunzi wawili.
Amesema kuwa hicho ni kiwango kikubwa cha maombi ya kisayansi ambacho hakijawahi kupokelewa miaka ya nyuma na ni matokeo ya mpango imara wa mafunzo ya kisayansi shuleni unaoendeshwa na YST katika mikoa yote nchini.
Ameongeza kwa mwaka huu umeshirikisha wanafunzi 6,064 na walimu wa sayansi 402 na kusisitiza mpango huo wa mafunzo ya kisayansi shuleni bado unaendelea na hatimaye zitachaguliwa kazi za sayansi 360 zitakazoendelea kupatiwa mafunzo katika duru ya pili.
Amesema lengo ni kuhakikisha kazi za sayansi zitakazoonyesha katika mashindano ya YST 2025 ni za ubora wa kiwango kinachoridhisha.”Kazi zo,” alisema Dk. Kamugusha
Aidha amesema kazi zote za kisayansi ambazo wanafunzi wanaendelea kuzifanyia utafiti kwa sasa zimejikita katika kutafiti njia za kutatua changamoto mbalimbali za maendeleo.
Hata hivyo Dk. Kamugisha amesema dhumuni la kufanya maonesho hayo UDSM ni kutengeneza jukwaa la kuwaleta pamoja wanasayansi chipukizi kutoka shule za sekondari la kuwakutanisha na wanasayansi wabobevu kutoka chuo hicho kikuu na vingine ili kupata ushauri juu ya namna bora ya kuboresha gunduzi zao.
“Mpango huu wa kuibua na kulea vipaji vya kisayansi kwa vijana unadhaminiwa na Karimjee Foundation (KFI) / Toyota Tanzania. Tunaamini kupitia mpango wetu huu vijana ambao ni wanasayansi chipukizi wataendelea kuhamasika zaidi katika kufanya gunduzi mbalimbali za kisayansi.” Alisema
Wakati huo huo Ofisa Mkuu wa Masoko Karimjee Foundation, Cobus van Zyl amefafanua kwamba tangu mwaka 2012 wamekuwa wadhamini Wakuu wa YST na kila mwaka wamekuwa wakitoa ufadhili wa masomo ya elimu ya juu kwa wanafunzi ambao wameshinda katika kundi la washindi wa jumla na kundi maalumu la elimu katika mashindano hayo.
Pia amesema fadhili huo haushii tu kwenye elimu bali unalenga kuboresha maisha ya kijana wa kitanzania na kwamba hadi sasa wahitimu 49 wa YST wamepokea ufadhili wa masomo kutoka Karimjee Foundation.
“Mafanikio haya ni fahari kubwa kwetu kuanzia katika taaluma za uhandisi na sayansi ya Afya hadi uhifadhi wa mazingira na sera. Ushirikiano huu ni mfano wa jitihada wa uwajibikaji wa Karimjee Foundation na YST ambao kwa pamoja unaonesha dhamira ya kukuza elimu nchini hususani sayansi na teknolojia kwa vijana.