Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Simon Chacha, amesisitiza umuhimu wa ujenzi wa skimu ya umwagiliaji kama hatua muhimu katika kuboresha sekta ya kilimo na kuinua maisha ya wakazi wa wilaya hiyo.
Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa utekelezaji wa mradi huo, amesema kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Tunduru na serikali inafanya juhudi za kutoa msaada kwa wakulima ili kuhakikisha shughuli za kilimo zinafanyika kwa usahihi na zinakuwa nguzo ya maendeleo ya wananchi.
“Skimu ya umwagiliaji itawawezesha wakulima kulima mazao mbalimbali kwa mwaka mzima bila kutegemea mvua, hivyo kuongeza uzalishaji wa mazao. alisema.
Mradi wa skimu ya umwagiliaji wa Mkotamo una thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 3.2, unatekelezwa kwa kipindi cha miezi 12 kuanzia Aprili 2025 hadi Aprili 2026, Ujenzi unajumuisha banio, mifereji mikuu na midogo mashambani, mifereji ya maji taka, pamoja na barabara za mashambani na vivusha maji kwaajili ya usafiri wa wakulima kuelekea mashambani.
Meneja wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji mkoani Ruvuma Lucia Chaula, ameongeza kuwa mradi huo utawanufaisha wakulima zaidi ya 497 na kuhamishia uzalishaji wa mazao kwenye hekari zaidi ya 867.
“Wananchi zaidi ya elfu 4 wa Mkotamo wanatarajiwa kunufaika moja kwa moja na mradi huu unaotarajiwa kukamilika mwezi Aprili 2026,” alisema Meneja Chaula. Ameongeza kuwa mazao yatakayopandwa ni pamoja na mpunga na mbogamboga.
Aidha, Chaula amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wakazi katika kulinda miundombinu ya mradi ili kuhakikisha unadumu na kuleta maendeleo endelevu.
“Ni muhimu kulinda banio, mifereji ya maji safi na maji taka pamoja na barabara, ili mradi uweze kufanikisha malengo yake kwa ustawi wa wakulima na jamii,” alisema.
Mkuu wa Wilaya na Meneja wa Tume ya Umwagiliaji wametoa wito kwa wakazi kushirikiana na kutumia rasilimali kwa njia bora na endelevu kwa kuzingatia kulinda vyanzo vya maji na mazingira.