Na Said Mwishehe,Tunduru
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Stephen Wasira amesema moja ya mafanikio katika miaka mine ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ni uwepo wa amani, umoja na mshikamano kwa Watanzania.
Aidha, amewahakikishia wananchi kuwa nchi iko salama huku akitumia nafasi hiyo kusisitiza kwamba Tanzania hakuna kubaguana kwa dini, rangi wala kabila.
Wasira ameyasema hayo leo Juni 10, 2025 alipokuwa akizungumza na wana CCM, wananchi, viongozi wa dini na makundi mbalimbali ya kijamii katika kikao cha ndani wilayani Tundurui, Mkoa wa Ruvuma.
Amesema Watanzania hawawezi kubaguana wala kugombana kwa sababu za kiimani kwa kuwa nchi yetu imeweka misingi mizuri ya uhuru wa kuabudu, hakuna anayezuiwa kwenda msikiti au kanisani.
“Sasa watu wa dini mbili wanaweza kugombana kwa sababu gani, tumesema kila mtu anasali na hakuna anayezuiwa. Ukienda msikitini hakuna aneyezuia, ukienda kanisa hakuna aliyezuiliwa wala kuulizwa.
“Tena ukiuliza ndugu zangu wa Kiislamu na ukiuliza Wakristo wote watakwambia chimbuko la dini zao ni Ibhrahimu, sasa Ibrahim kasema mgombane?
“Sisi wote chimbuko moja tena mimi si msomi wa Koraan lakini ukiwaikiliza Koraan na ukasoma Torati katika Agano la Kale utakuta wanazungumza lugha ile ile, wote wanamwamini Mungu mmoja, sasa Mungu mmoja alisema tugombane au tumuabudu…” alieleza na kuhoji.
Amesisitiza Tanzania imejengwa kuwa nchi ya watu wenye umoja ambao hawagombani kwa makabila, hawabuguani kwa dini na hayo ni mambo nadra kuyakuta katika nchi nyingi barani Afrika.